Wednesday, November 12, 2014

Serikali kudhibiti ukimwi hadi kufikia maambukizi sifuri

Na Genofeva Matemu – Maelezo

Serikali imepanga mikakati na kusimamia juhudi zinazofanywa na kuendelezwa na wadau wa ukimwi kuhakikisha kuwa maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi yanapungua hadi kufikia sifuri ifikapo mwaka 2025.

Kauli hiyo imetolewa na mwenyekiti mtendaji kutoka Tume ya kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS) Dkt. Fatma H. Mrisho wakati wa mkutano wa serikali na wadau wa ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi jana jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa mkutano huo Dkt. Mrisho amesema kuwa maambukizi ya ukimwi yamepungua ukilinganisha na miaka 10 iliyopita kwani idadi imepungua kutoka waathirika laki moja na elfu themanini hadi kufikia waathirika elfu sabini na mbili kwa sasa.

Akitoa mfano Dkt. Mrisho amesema kuwa Mkoa wa Njombe, Shinyanga, Dar es Salaam, Mbeya na Rukwa ni mikoa ambayo inaonyesha kuwa na idadi kubwa ya waathirika wa ukimwi hivyo kuwataka wadau wa ukimwi kutoka mikoa hiyo kutoa elimu ya kutosha kwa jamii ili kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi pamoja na magojwa ya zinaa.

Akifungua mkutano huo, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. Florens Turuka amesema kuwa serikali imedhamiria kuanzisha mfuko utakaokua unashughulikia masuala ya ukimwi wakati wa bajeti ya mwaka 2015/2016 wenye lengo la kuondoa maambukizi mapya ya ukimwi nchini.

Aidha Dkt. Turuka ameitaka jamii kutowanyanyapaa waathirika wa ukimwi bali wawapende na kuwapa moyo ili waendelee kuwa na afya bora kwani serikali inawapigania na kuhakikisha kuwa wanatumia dawa za kuongeza maisha ili kupunguza vifo vinavyotokana na ugonjwa huo.

Mkutano wa serikali na wadau wa ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi ulianzishwa mwaka 2003 ukifuatiwa na ule wa mwaka 2006 na kuendelezwa kila baada ya miaka miwili ambapo mkutano wa mwaka huu ni wa sita na umebeba kauli mbiu inayosema “Kwa yale mafanikio ambayo tumeyapata mpaka sasa tunayaendeleza”.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. Florens Turuka akifungua Mkutano wa Serikali na wadau wa Ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi jana jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Dkt. Fatma Mrisho akizungumza na wadau mbalimbali walioshiriki Mkutano wa Serikali na wadau wa Ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi jana jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa wadau wa Maendeleo kwenye sekta ya ukimwi Dkt. Michelle Roland akiwasilisha mada wakati wa Mkutano wa Serikali na wadau wa Ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi jana jijini Dar es Salaam.
Wadau mbalimbali walioshiriki Mkutano wa Serikali na wadau wa Ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi wakifuatilia kwa makini mada zilizokua zikitolewa kuhusu kupunguza maambukizi ya ukimwi hadi kufikia sifuri.
Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Dkt. Fatma Mrisho katikati akijadili jambo na mgeni rasmi Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. Florens Turuka kushoto. Kulia ni Mwenyekiti wa wadau wa Maendeleo kwenye sekta ya ukimwi Dkt. Michelle Roland.
Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) Dkt. Fatma Mrisho akimpongeza kijana Yohana Haule mwenye umri wa miaka 23 kwa kuchora nembo na kupata tuzo ya kimataifa ya AIDS.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Dkt. Florens Turuka aliyekaa katikati kwenye picha ya pamoja na Wadau mbalimbali walioshiriki Mkutano wa Serikali na wadau wa Ukimwi kupitia utekelezaji wa programu za ukimwi. Picha na: Genofeva Matemu - Maelezo

No comments:

Post a Comment