Wednesday, May 9, 2012

CCTV ZAMFICHUA MWIZI WA PESA CRDB



 
MKAZI wa Sinza Kijiweni aliyefahamika kwa jina moja la Ali ametiwa mbaroni na askari polisi, kwa kwa tuhuma za kuwaibia pesa wateja wa Benki ya CRDB tawi la Makumbusho lilipo  jengo la Milllenium Tower.

Mashuhuda wa tukio hilo waliliambia Mwananchi kuwa mtuhumiwa huyo alinaswa jana akiwaibia wateja wa benki hiyo ndani ya benki, wakati wakijaza fomu za kuweka pesa.

Mmoja wa watu hao walioshuhudia tukio hilo, David Nyamwelo aliliambia Mwananchi kuwa mtuhumiwa huyo aliweza kukamatwa akifanya uhalifu huo kwa msaada wa kamera za usalama zilizofungwa ndani ya benki hiyo.

“Kuna dada mmoja alikuwa akijaza fomu ya kuweka pesa  huku akiwa ameweka pesa juu ya meza akiwa amezitenga katika mafungu kadhaa ya noti kuanzia  za Sh.10,000, 5,000 na 2,000,” alisema Nyamwelo na kuongeza;
"Wakati akiendelea kujaza na huyo jamaa (mtuhumiwa) alikuwa amesimama pembeni yake katika meza hiyo hiyo, na wakati dada huyo alipogeuka tu jamaa akachomoa Sh.30,000."

Alisema baadaye  dada huyo alipohesabu akakuta zimepungua lakini, akahisi kuwa labda alikuwa amechanganya kuhesabu akiwa nyumbani.

Alisema baada ya mfanyakazi mmoja wa benki hiyo anayeratibu kamera za usalama katika benki hiyo kuingia katika chmba cha kamera, akaliona tukio hilo.

Shuhuda huyo aliendelea kueleza kuwa baada ya kuona tukio hilo, mfanyakazi huyo alimtuma mwenzake aende kaunta ili kumwangalia mtu huyo lakini baadaye yule mratibu wa kamera akamuona yule mtuhumiwa akichomoa pesa kwa mteja mwingine.

“Hivyo ilibidi wamfuatile hadi pale kaunta na wakamkuta huyo jamaa na kumtia mbaroni kisha wakamkabidhi kwa askari polisi wanaolinda katika benki,” alisema shuhuda huyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Charles Kenyela alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo kwanza alisema alikuwa hajapata taarifa hizo kwa kuwa yuko likizo lakini, aliahidi kufuatilia.

No comments:

Post a Comment