Saturday, May 17, 2014

Ziara ya Goodluck Chibok yafutiliwa mbali


Jeshi la Nigeria linakumbwa na hali ngumu kuweza kudhibiti wapiganaji wa Boko Haram
Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan amefutilia mbali ziara yake katika mji wa Chibok ambako zaidi ya wasichana miambili wametekwa nyara na kundi la Boko Haram.
Duru zinasema kuwa ziara ya Rais Goodluck alifutilia mbali ziara yake kwa sababu za kiusalama.
Rais alitarajiwa kuzuru mji huo huku wengi wakimkosoa kwa kuchelewesha juhudi za kuokolewa kwa wasichana hao waliotekwa nyara mwezi mmoja iliopita.
Kufutiliwa mbali kwa ziara hiyo ni ishara tosha ya hali ya usalama ilivyo mbovu katika eneo la Kaskazini Mashariki mwa nchi.
Rais Goodluck Jonathan amekosolewa vikali kwa kujikokota katika kupatia kipaombele juhudi za kuwanusuru wasichana hao
Hii leo anatarajiwa kwenda mjini Paris,Ufaransa ambako atahudhuria mkutano kuhusu namna ya kukabiliana na kundi la Boko Haram ambao utahudhuriwa na viongozi kutoka kanda ya Afrika Mashariki na Magharibi, Marekani na Ulaya.
Bunge la Nigeria wiki hii lilipigia kura hoja ya kuongeza muda wa sheria ya hali ya hatari katika majimbo matatu ambako jeshi limekuwa likipigwa na wapiganaji wa Boko Haram.
Maafisa wa serikali wamekuwa wakiwasihi wakazi kuunda makundi ya kutoa ulinzi kwa maeneo wanakoishi na pia ili kuweza kusaidia jeshi kupambana na Boko Haram.

No comments:

Post a Comment