Wednesday, October 5, 2016

PLAN INTERNATIONAL YAJIPANGA KUADHIMISHA SIKU YA MSICHANA KWA KISHINDO


Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Plan International, Jorgen Haldorsen akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam (hawapo pichani) juu ya maadhimisho ya siku ya Msichana Duniani itakayoadhimishwa Octoba 11 mwaka huu katika mikoa ambayo shirika hilo linafanya kazi.(Picha zote na Jacquiline Mrisho - Maelezo)
Msichana atakayekaimu nafasi ya Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Plan International, Catherine Kapilima akiongea na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam (hawapo pichani) namna alivyoipokea na atakavyoitumia nafasi hiyo ikiwa ni moja ya kuadhimisha siku ya Msichana Duniani Octoba 11 mwaka huu katika Mikoa ambayo shirika hilo linafanya kazi.

Na Jacquiline Mrisho - Maelezo
SHIRIKA la Plan International limejipanga kuadhimisha Siku ya Msichana Duniani kwa kuwakabidhi wasichana madaraka katika ofisi zao ili waweze kuonyesha uwezo wao wa kufanya maamuzi katika masuala mbalimbali.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika hilo, Jorgen Haldorsen alipokuwa akiongea na waandishi wa habari juu ya maadhimisho ya siku hiyo yatakayofanyika Octoba 11 mwaka huu katika Mikoa ambayo shirika hilo linafanya kazi.

Haldorsen amesema kuwa Shirika hilo litaungana na mataifa mengine katika kusimamia usawa na kumpa msichana nafasi ya kujifunza, kuongoza na kutoa maamuzi yaliyo bora ili kuwapa fursa sawa bila kujali jinsia.

“Kwa kuelekea kilele cha Siku ya Msichana Duniani, Ofisi zote za Shirika letu pamoja na wadau wetu wakiwemo ubalozi wa Kanada tumeamua kuadhimisha siku hii kwa kuwakaimisha uongozi baadhi ya wasichana hivyo, tunatoa rai kwa mamlaka zingine kuwaachia wasichana nafasi ili waone uwezo wao wakiwa kwenye mamlaka mbalimbali”, alisema Haldorsen.

Mkurugenzi huyo ameyataja matukio mengine ambayo yatafanyika katika maadhimisho hayo yakiwemo ya kuzindua miradi ya kuzuia ndoa za utotoni katika Mikoa ya Rukwa na Morogoro pamoja na kufanya majadiliano ya moja kwa moja kati ya Mke wa Rais wa Amerika, Mitchel Obama na wasichana 25 wa shirika la plan International kutoka katika nchi 3 za Tanzania, Peru na Cambodia.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Ulinzi wa Watoto, Jane Mrema amesema kuwa wasichana wamekuwa wakipambana na vikwazo vingi vinavyowazuia kupata fursa mbalimbali katika jamii hivyo nguvu ya ziada inatakiwa katika kuhakikisha mawazo hayo potofu yanakoma.

“Tukijitahidi kuondoa vikwazo vinavyowakabili wasichana na kuwapa nafasi wanaweza kuleta mabadiliko makubwa, kinachotakiwa ni kuwaamini na kuwapa fursa sawa na wengine”, alisema Mrema. 

Naye msichana atakayekaimu nafasi ya Mkurugenzi Mkazi wa Shirika hilo, Catherine Kapilima amesema kuwa kitendo cha kuachiwa madaraka hayo kitamjengea uwezo wa kufanya kazi kwa vitendo pamoja na kuwashawishi wasichana wenzie kuamini kuwa kila kitu kinawezekana bila kujali jinsia.

Siku ya Msichana Duniani inaadhimishwa kwa lengo la kuonesha vizuizi mbalimbali kwa maendeleo ya wasichana na jinsi ya kuvitatua, huadhimishwa Octoba 11 kila mwaka. Hii ni mara ya tano kuadhimishwa.

No comments:

Post a Comment