Thursday, March 30, 2017

WATANZANIA WATAKIWA KUJITOLEA KUCHANGIA DAMU


Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo Dkt. Bashir Nyangasa  akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambi ya siku tatu ya upasuaji wa Moyo katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) ambapo madaktari wa JKCI walishirikiana na Madaktari 6 kutoka nchini India. Madaktaria hao wamekuja nchini kufuatia ahadi ya Kiongozi Mkuu wa Madhehebu ya Mabohora Duniani Mtakatifu Syedana Muffadal Saifuddin Saheb kwa Rais Dkt. Magufuli alipomtembelea Ikulu Jijini Dar es Salaam mapema tarehe 13, Oktoba 2016.Kushoto ni Mwakilishi Mkazi wa Madhehebu ya Mabohora nchini Sheikh Tayabali Hamzabhai.

Frank Mvungi-Maelezo
WATANZANIA wametakiwa kujitolea kuchangaia Damu ili kuwasaidia wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji wa moyo wanaohitaji kuongezewa damu wakati wa kupatiwa matibabu.

Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Upasuaji wa Moyo na Daktari Bingwa wa Moyo Dkt. Bashir Nyangasa kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam.

“Tunatarajia kuwa na kambi maalum ya matibabu ya moyo kwa watoto itakayoanza tarehe 3/4/2017 hadi tarehe 7/4/2017 ambapo Taasisi yetu itashirikiana na Madaktari Bingwa kutoka Taasisi ya Healinga Little ya London Uingereza.”Alisisitiza Dkt. Nyangasa.

Akifafanua Nyangasa amesema kuwa wagonjwa 12 wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji katika kipindi hicho kwa ushirikiano na Madaktari hao kutoka Taasisi ya Healing Little ya London Uingereza.

Kufuatia upasuaji huo Dkt. Nyangasa amewaomba wananchi kuendelea kuchangia damu  ili kusaidia kuokoa maisha ya wale wanaohitaji kuongezewa damu.

Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete imekuwa Moja ya Taasisi Bora katika ukanda wa Afrika mashariki na Kati katika kutoa matibabu moyo kwa wagonjwa kutoka hapa nchini na katika mataifa mbalimbali yanayoizunguka Tanzania.


Upatikanaji wa damu yakutosha imekuwa moja ya changamoto zinazoikabili Sekta ya afya kutokana na mwitikio mdogo wa wananchi kujitolea damu ili kusaidia wale wenye uhitaji hivyo ni wajibu wa kila mtanzania kuunga mkono juhudi za Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete katika kuhamasisha wananchi kujitolea kuchangia damu.

No comments:

Post a Comment