Sunday, June 24, 2012

‘Madaktari chonde msigome’

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Mwinyi
 
Serikali imetoa tahadhari kwa madaktari nchini kuachana na mpango wao wa mgomo unaotarajia kuanza leo kwani utagharimu maisha ya watu wasio na hatia na kwenda kinyume na sheria na kiapo chao cha kazi.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Mwinyi, alitoa tahadhari hiyo jana alipokuwa akitoa kauli ya mawaziri bungeni mjini Dodoma.

Alisema hiyo inatokana na madhara yatokanayo na mgomo wa madaktari kuwa ni makubwa na yanayogharimu maisha ya watu moja kwa moja, tofauti na migomo inayofanywa na kada nyingine za wafanyakazi.

Hata hivyo, alisema kabla ya kuendelea na mpango huo, hawana budi kufikiria kwa kina ili kuepuka madhara ambayo yatagharimu maisha ya Watanzania wasio na hatia.

“Serikali muda wote imeonyesha nia njema ya kujadiliana na uongozi wa madaktari ili kutafuta ufumbuzi wa masuala waliyoyawasilisha kwa kuzingatia uwezo wa serikali,” alisema.

Alisisitiza kuwa serikali imejitahidi kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma za afya nchini kwa hatua mbalimbali kama kununua vitendea kazi na vifaa tiba, kufanyia ukarabati hospitali mbalimbali zikiwemo za rufaa.

Aliwasihi madaktari kukubaliana na mapendekezo yaliyotolewa na serikali kwa kuwa bado ina nia ya kuboresha mazingira ya kazi zao na kuyapatia ufumbuzi madai yao ili kuwepo na ufanisi katika utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi kadri ya uwezo wao.

Juzi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati akijibu swali la Mbunge wa Hai (Chadema), Freeman Mbowe, alisema timu iliyoundwa kushughulikia mgogoro huo, haikukubaliana katika mambo matano kati ya 10, ambayo ni posho ya usafiri, nyumba, mazingira magumu ya kazi na nyongeza ya mishahara na hivyo kuona lifikishwe Mahakama ya Usuluhishi (CMA).

Hata hivyo, CMA iliamua kuwa jambo hilo lifikishwe katika Mahakama ya Kazi.

MADAKTARI SHINYANGA NA SIMIYU: HATUJAAMUA KUGOMA

Madaktari wa mikoa ya Simiyu na Shinyanga wamesema hawatapenda kuona mgonjwa anapoteza maisha au magonjwa na matatizo yanayoweza kuzuilika akifa kipindi hiki ambacho kuna mgomo.

Akizungumzia kuanza kwa  mgono wa madakairi nchi nzima leo Mganga Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Dk Costa Mniko, alisema kuwa madaktari na wauguzi katika mkoa wa Shinyanga na mkoa wa Simiyu ambao pia yeye anaulea kama mganga mkuu alisema kamwe hawatakuwa katika mgomo kama inavyotarajiwa.

Dk Mniko aliiambia NIPASHE mjini Bariadi jana muda mfupi baada ya uzinduzi wa Mradi wa Uzazi Uzima katika mkoa mpya wa SimIyu.

Alisema madaktari wa mikoa hiyo hawajapata barua au maandishi ya kuwataka washiriki katika mgomo uliotangazwa nchini nzima na kuwa nikuwaonea wananchi hasa wale wa vijijini.

Akifafanua juu ya mgomo huo mganga mkuu huyo alisema kuwa kunahitajika kutumia busara kwanza kabla ya kufikia uamuzi wa kugoma kumhudumia mgonjwa aliyeko mbele yako na kuongeza kuwa mgonjwa ndiye hasa ajira ya Udaktari na hata kumpatia wadhifa na taaluma hiyo.

Mniko alisema kuwa kunahitajika busara na huruma kwanza kwa mgonjwa na kumwacha akifa huku akikulilia umpe matibabu na anapokufa ukimwona ni jambo baya sana kwa daktari yeyote anayejua taaluma yake.

Alipohojiwa utayari wao juu ya kuunga mono mgomo huo pindi wakipata barua au maadishi ya kuwata kufanya hivyo,mkuu huyo alisema kuwa ipo haja ya kukutana na madaktari wenzake na timu nzima ya uongozi wa afya
kujadili juu ya faida ya mgomo huo na kuona ninani wa kulaumiwa mgonjwa au serikali.

Hata hivyo mganga huyo alitia mashaka kuwa huenda mgomo huo ukawa na mlengo wa kisiasa kuliko taaluma ilivyo.

Mkoa wa Shinyanga unajumisha wilaya za Kahama, Shinyanga na Kishapu nau mkoa mpya wa Simiyu ukijumisha wilaya za  Meatu, Maswa, Itilima, Bariadi na Busega.

MSIMAMO WETU UKO PALE PALE

Jumuiya na Madaktari nchini imesema kuwa msimamo wao uko pale pale wa kufanya mgomo kwani hakuna makubaliano yoyote waliyoafikiana mpaka sasa licha ya serikali kudai wameafikiana.

Akizungumza na NIPASHE jana jijini Dar es Salaam, Kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka, alisema kuwa alichokizungumza Waziri wa Afya na Utawi wa Jamii, Dk. Hussen Mwinyi ni kulipotosha bunge na kwamba hakuna makubaliano yoyote aliyofanya na madaktari.

Alisema kama Dk. Mwinyi alikutana na Chama cha Madaktari (MAT) na kukubaliana nao katika madai ya madaktari haikuwa sahihi kwani mgogoro huo upo chini ya madaktari na sio MAT.

"Kama suala la mahakamani watapelekana MAT na serikali na sio madaktari kwa kuwa ndio waliokubaliana na mgomo wetu uko pale pale kwani makubaliano hayo ambayo ameyaeleza Dk. Mwinyi hayakuwa makubaliano na madaktari," alisema Dk. Ulimboka.

Dk. Ulimboka alisema sakata la mgogoro huo lipo chini ya madaktari kupitia jumuiya ambayo imeteuliwa ili kushughulikia suala hilo na sio chama cha MAT, hivyo tamko letu haliwezi kubadilika mpaka hapo serikali itakapokubali kushughulikia madai yetu.

Taarifa hii imeandaliwa na Sharon Sauwa, Dodoma, Ancent Nyahore, Shinyanga na Beatrice Shayo, Dar es Salaam.

 WANANCHI WANASEMAJE?

Kwa upande wake, Mkazi wa Mwananyama, Hamis Mohamed, alisema amesikitishwa na kitendo cha serikali kutotekeleza madai ya madaktari hali ambayo imewafanya watangaze kuanza kwa mgomo mwingine.

Alisema wananchi wamekuwa wakipata madhara makubwa kwa kuwa wamekuwa wakizitegemea hospitali hizo kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na hospitali za watu binafsi kwani gharama zipo juu hali inayowafanya washindwe kwenda kupatiwa matibabu.

Mohamed alisema serikali ingetakiwa kuliangalia suala hilo kwa kina kupitia mgomo wa mwanzo ambao ulisababisha madhara makubwa ambapo vifo vingi vilitokea kutokana na tatizo hilo.

"Sisi wa kima cha chini ndio tunapata tabu wenzetu viongozi  pamoja na watoto wao wanajitibu katika hospitali kubwa tena za binafsi sisi tunaendelea kujifia huduma bado ni mbaya unaenda hospitali unakosa dawa huku unakuta mgonjwa wako yupo katika hali mbaya  serikali inaendelea kupigana vijembe bungeni," alisema.

Alisema muda umekwisha wa kupeana vijembe kinachotakiwa ni utekelezaji wa madai ya madaktari ili wawe wanapatiwa huduma bora zinazoenda na kiwango kinachotakiwa.

Naye Agatha Kessy alisema madaktari ni haki yao kugoma kwa yale waliyoahidi yameshindwa kutekelezeka, hivyo serikali iwatimizie ili waweze kufanya kazi katika mazingira bora kwani madai yao yalikuwa ni ya msingi.

Alisema pamoja na kwamba mgomo huo utawasababishia wananchi matatizo ni kwamba hakuna jinsi kwani serikali ndiyo iliyozembea katika suala hilo.

"Serikali ilishaahidi suala hilo la mgomo halitajirudia sasa iweje ishindwe kuwapatia haki zao wakati taalum hiyo haitakiwi kuchezewa hao ni watu muhimu sana na wanatakiwa waheshimiwe ili watupatie huduma bora," alisema Kessy

Kessy alisema tatizo kubwa ambalo limejitokeza katika sakata hilo ni kwamba serikali inalichukulia jambo hilo kisiasa na ndio maana imeshindwa kutekeleza madai ya madaktari.

No comments:

Post a Comment