Wednesday, June 27, 2012

Moi yatangaza kusitisha huduma



TAASISI ya  Mifupa Muhimbili (MOI) imetangaza rasmi kusitisha baadhi ya huduma zake kutokana na mgomo wa madaktari unaoendelea nchini na kushika kasi zaidi katika hospitali za rufaa za KCMC, Bugando na Mbeya

Wakati mgomo huo ukileta athari hizo, Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi imekionya Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) kuhusu utekelezaji wa amri yake ya kusitisha mgomo wao na kukiagiza rasmi kutangaza kusitisha mgomo huo kupitia vyombo vya habari, hadi Julai 24, 2012.
Onyo na amri hiyo ilitolewa jana na Jaji Sekela Moshi kwa Rais wa MAT akirejea amri aliyoitoa Ijumaa iliyopita akikiagiza chama hicho na wanachama wake kutoitisha mgomo wala kushiriki katika mgomo huo.

Jaji Sekela alitoa amri hiyo kufuatia maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na Serikali ikiomba mahakama isikilize na kutoa uamuzi wa upande mmoja wa kuzuia mgomo huo kwa muda kusubiri usikilizwaji wa pande zote wa maombi hayo.

Amri hiyo ya jana ilikuwa inakazia nyingine ambayo ilitolewa Ijumaa iliyopita, siku ambayo chama hicho kilitangaza kuanza kwa mgomo siku inayofuta.
Hata hivyo amri hiyo haikutekelezwa na chama hicho na kulikuwepo na madai kwamba viongozi hawakupatiwa nakala ya amri hiyo.


MOI

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, msemaji wa Taasisi hiyo, Jumaa Almas alisema taasisi imelazimika kusitisha baadhi ya huduma kutokana na kukabiliwa na upungufu wa madaktari kwani wengi wapo kwenye mgomo.

"Hali halisi ni kwamba tumesitisha huduma kwa baadhi ya vitengo, hii inatokana na upungufu wa madaktari wanaofanya kazi katika Taasisi hii, wengi wapo kwenye mgomo na wanaofanya kazi kwa sasa ni wakuu wa Idara," alisema Almas.
Almas alitaja huduma zilizosimamishwa kuwa ni za upasuaji na uchunguzi binafsi kwa wagonjwa huku akitaja vitengo vinavyoendelea kufanya kazi kuwa ni huduma za kawaida, wagonjwa wa wodini na kitengo cha huduma za dharura.

KCMC

Hali ya utoaji huduma katika hospitali ya Rufaa ya KCMC inayoendeshwa na shirika la kidini la msamaria mwema (GSF) imezidi kuzorota baada ya madaktari karibu 80 kugoma kurejea kazini.

Baadhi ya wagonjwa waliokuwa wamepewa rufaa kutoka hospitali mbalimbali kwenda KCMC, jana walijikuta wakirudishwa walikotoka kutokana na mgomo wa madaktari unaoendelea hospitalini hapo.

Mbali na kutopokelewa kwa wagonjwa wapya wanaohitaji kulazwa, kliniki zote za wagonjwa wa kisukari, ukimwi na wale waliofanyiwa oparesheni zimefungwa rasmi kutoa huduma kwa wagonjwa.

“Huduma kwa wagonjwa wanaotoka nje zimesimama wanaohudimiwa ni wale ambao mgomo umewakuta ndani na wale wagonjwa waliozidiwa tu,” alieleza mmoja wa madaktari bingwa katika hospitali hiyo.

Madaktari ambao wamejitoa mhanga kwa kutoingia wodini toka juzi mchana ni wale walioko katika mafunzo kwa vitendo huku wanaosomea udaktari bingwa wakiwa njiapanda.

“Madaktari walioko kwenye majaribio hawajarejea kazini na wanaotoa huduma ni madaktari bingwa wakisaidiana na wale wanaosomea ubingwa ambao wako kama hawako,” alidokeza daktari mmoja.

Jitihada za kumpata Mkurugenzi wa KCMC, Dk Moshi Ntabaye kuelezea mgomo huo licha ya kusota katika hospitali hiyo tangu asubuhi zilishindikana hadi ilipotimu saa 10:00 mchana.

Mbeya

Mkoani Mbeya, mgomo wa madaktari umeingia sura mpya  baada ya madaktari  64 katika Hospitali ya Rufaa kukaidi kukaa meza moja na  bodi ya hospitali hiyo chini ya Mwenyekiti wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro.

Bodi hiyo iliwaandikia madakatari hao barua jana kuwataka wakutane kwa lengo la kujadili mgomo huo ambao unawahusisha madari madkatari 64 wakiwemo 19 waajiriwa na 45 wa mafunzo kwa vitendo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Dk Norman Sigalla alisema Bodi hiyo imedhamiria  kusitisha mikataba ya madaktari waliogoma hasa wale ambao wako kwenye mafunzo ya vitendo na kuwarejesha wizarani.

Alisema kuwa Bodi imefikia hatua hiyo baada ya kuona kuwa madaktari hao wamevunja mkataba wao ambao unawataka kufanya kazi bila kugoma na kukaidi wito wa bodi wa kuwataka kukaa pamoja na kufanya mazungumzo kuhusu mgomo huo.

“Tuliwaandikia barua kila mmoja ya kuwaita waje ili tuzungumze nao, lakini hawakuja hata mmoja, hivyo tumewapa barua nyingine ili wajieleze kwa nini tusiwachukulie hatua na kama hawatarejea kazini hadi kesho (leo) tutalazimika kusitisha mikataba yao na kuwarejesha wizarani,” alisema Dk Sigalla.

Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Mbeya, Dk Eliuter Samky alisema kuwa madhara yaliyosababishwa na mgomo huo kwa wagonjwa wote waliofikishwa hospitalini hapo tangu  mgomo huo ulipoanza kwa madaktari hao waliathirika kwa namna moja au nyingine.

“Idadi ya akinamama wanaohitaji kujifungua imeongezeka mara dufu kwenye hospitali yetu ya mkoa kutokana na huduma kukosekana kwenye hospitali ya wazazi Meta, hali hii imesababisha hospitali ya Mkoa kuelemewa kiasi cha akina mama wengine kulala chini,” alisema Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Seif Mhina

Mwananyamala

Hospitali ya Mwananyamala huduma za afya ziliendelea kutolewa kwa wagonjwa waliofika kupata huduma hiyo huku kukiwa hakuna dalili zozote za mgomo.

“Kwanza sijui kama kunamgomo kwani nimehudumiwa bila wasiwasi na sasa naondoka nyummbani,” alisema Mwajuma Sadiki.

Temeke

Hali ya matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke zinaendelea vizuri licha ya baadhi ya  hospitali madaktari wao kugoma.

Mmoja ya wananchi aliyejitambulisha kwa jina la Said Suleiman alisema kuwa madaktari katika hospitali hiyo wanafanya kazi kama kawaida na hakuna dalili zozote za mgomo kutokea.

“Mwanangu alikuwa amelazwa takribani siku tatu na leo saa 6 ameruhusiwa kurudi nyumbani baada ya hali yake kuridhisha kwa kweli madaktari wameonyesha ushirikiano mzuri mpaka kufikia hatua hii,” alisema Suleimani.

Suleiman alisema licha ya madaktari hao kutoonyesha nia ya kugoma ila wamekuwa wakiendekeza vitendo vya rushwa jambo ambalo limekuwa likiwasumbua wakazi mbalimbali wanaofika kupata huduma hiyo hospitalini hapo.

Mwananchi ambaye hakutaka kutaja jina lake alisema kuwa tangu kutangazwa kwa mgomo huo Juni 23 mwaka huu yeye hajaona dalili zozote katika hospitali hiyo ila jambo ambalo linalowasikitisha ni vitendo vya rushwa vinavyoendelea hapo.

“Sikufichi madaktari wa hapa wanahudumia ila kama huna fedha utapata shida kwa kiasi fulani na kupelekea mgonjwa wako kuchukua muda kupata matibabu,” alisema.

No comments:

Post a Comment