TAASISI
ya Mifupa Muhimbili (MOI) imetangaza rasmi kusitisha baadhi ya huduma
zake kutokana na mgomo wa madaktari unaoendelea nchini na kushika kasi
zaidi katika hospitali za rufaa za KCMC, Bugando na Mbeya
Wakati
mgomo huo ukileta athari hizo, Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi imekionya
Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) kuhusu utekelezaji wa amri yake ya
kusitisha mgomo wao na kukiagiza rasmi kutangaza kusitisha mgomo huo
kupitia vyombo vya habari, hadi Julai 24, 2012. Onyo na amri hiyo
ilitolewa jana na Jaji Sekela Moshi kwa Rais wa MAT akirejea amri
aliyoitoa Ijumaa iliyopita akikiagiza chama hicho na wanachama wake
kutoitisha mgomo wala kushiriki katika mgomo huo.
Jaji Sekela
alitoa amri hiyo kufuatia maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na
Serikali ikiomba mahakama isikilize na kutoa uamuzi wa upande mmoja wa
kuzuia mgomo huo kwa muda kusubiri usikilizwaji wa pande zote wa maombi
hayo.
Amri hiyo ya jana ilikuwa inakazia nyingine ambayo
ilitolewa Ijumaa iliyopita, siku ambayo chama hicho kilitangaza kuanza
kwa mgomo siku inayofuta. Hata hivyo amri hiyo haikutekelezwa na chama hicho na kulikuwepo na madai kwamba viongozi hawakupatiwa nakala ya amri hiyo.
MOI
Akizungumza
na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, msemaji
wa Taasisi hiyo, Jumaa Almas alisema taasisi imelazimika kusitisha
baadhi ya huduma kutokana na kukabiliwa na upungufu wa madaktari kwani
wengi wapo kwenye mgomo.
"Hali halisi ni kwamba tumesitisha
huduma kwa baadhi ya vitengo, hii inatokana na upungufu wa madaktari
wanaofanya kazi katika Taasisi hii, wengi wapo kwenye mgomo na
wanaofanya kazi kwa sasa ni wakuu wa Idara," alisema Almas. Almas
alitaja huduma zilizosimamishwa kuwa ni za upasuaji na uchunguzi binafsi
kwa wagonjwa huku akitaja vitengo vinavyoendelea kufanya kazi kuwa ni
huduma za kawaida, wagonjwa wa wodini na kitengo cha huduma za dharura.
KCMC
Hali
ya utoaji huduma katika hospitali ya Rufaa ya KCMC inayoendeshwa na
shirika la kidini la msamaria mwema (GSF) imezidi kuzorota baada ya
madaktari karibu 80 kugoma kurejea kazini.
Baadhi ya wagonjwa
waliokuwa wamepewa rufaa kutoka hospitali mbalimbali kwenda KCMC, jana
walijikuta wakirudishwa walikotoka kutokana na mgomo wa madaktari
unaoendelea hospitalini hapo.
Mbali na kutopokelewa kwa wagonjwa
wapya wanaohitaji kulazwa, kliniki zote za wagonjwa wa kisukari, ukimwi
na wale waliofanyiwa oparesheni zimefungwa rasmi kutoa huduma kwa
wagonjwa.
“Huduma kwa wagonjwa wanaotoka nje zimesimama
wanaohudimiwa ni wale ambao mgomo umewakuta ndani na wale wagonjwa
waliozidiwa tu,” alieleza mmoja wa madaktari bingwa katika hospitali
hiyo.
Madaktari ambao wamejitoa mhanga kwa kutoingia wodini toka
juzi mchana ni wale walioko katika mafunzo kwa vitendo huku wanaosomea
udaktari bingwa wakiwa njiapanda.
“Madaktari walioko kwenye
majaribio hawajarejea kazini na wanaotoa huduma ni madaktari bingwa
wakisaidiana na wale wanaosomea ubingwa ambao wako kama hawako,”
alidokeza daktari mmoja.
Jitihada za kumpata Mkurugenzi wa KCMC,
Dk Moshi Ntabaye kuelezea mgomo huo licha ya kusota katika hospitali
hiyo tangu asubuhi zilishindikana hadi ilipotimu saa 10:00 mchana.
Mbeya
Mkoani
Mbeya, mgomo wa madaktari umeingia sura mpya baada ya madaktari 64
katika Hospitali ya Rufaa kukaidi kukaa meza moja na bodi ya hospitali
hiyo chini ya Mwenyekiti wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro.
Bodi
hiyo iliwaandikia madakatari hao barua jana kuwataka wakutane kwa lengo
la kujadili mgomo huo ambao unawahusisha madari madkatari 64 wakiwemo
19 waajiriwa na 45 wa mafunzo kwa vitendo.
Akizungumza kwa niaba
ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Dk Norman Sigalla
alisema Bodi hiyo imedhamiria kusitisha mikataba ya madaktari waliogoma
hasa wale ambao wako kwenye mafunzo ya vitendo na kuwarejesha wizarani.
Alisema
kuwa Bodi imefikia hatua hiyo baada ya kuona kuwa madaktari hao
wamevunja mkataba wao ambao unawataka kufanya kazi bila kugoma na
kukaidi wito wa bodi wa kuwataka kukaa pamoja na kufanya mazungumzo
kuhusu mgomo huo.
“Tuliwaandikia barua kila mmoja ya kuwaita waje
ili tuzungumze nao, lakini hawakuja hata mmoja, hivyo tumewapa barua
nyingine ili wajieleze kwa nini tusiwachukulie hatua na kama hawatarejea
kazini hadi kesho (leo) tutalazimika kusitisha mikataba yao na
kuwarejesha wizarani,” alisema Dk Sigalla.
Mkurugenzi wa
Hospitali ya Rufaa Mbeya, Dk Eliuter Samky alisema kuwa madhara
yaliyosababishwa na mgomo huo kwa wagonjwa wote waliofikishwa
hospitalini hapo tangu mgomo huo ulipoanza kwa madaktari hao
waliathirika kwa namna moja au nyingine.
“Idadi ya akinamama
wanaohitaji kujifungua imeongezeka mara dufu kwenye hospitali yetu ya
mkoa kutokana na huduma kukosekana kwenye hospitali ya wazazi Meta, hali
hii imesababisha hospitali ya Mkoa kuelemewa kiasi cha akina mama
wengine kulala chini,” alisema Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Seif
Mhina
Mwananyamala
Hospitali ya Mwananyamala huduma za
afya ziliendelea kutolewa kwa wagonjwa waliofika kupata huduma hiyo huku
kukiwa hakuna dalili zozote za mgomo.
“Kwanza sijui kama kunamgomo kwani nimehudumiwa bila wasiwasi na sasa naondoka nyummbani,” alisema Mwajuma Sadiki.
Temeke
Hali ya matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke zinaendelea vizuri licha ya baadhi ya hospitali madaktari wao kugoma.
Mmoja
ya wananchi aliyejitambulisha kwa jina la Said Suleiman alisema kuwa
madaktari katika hospitali hiyo wanafanya kazi kama kawaida na hakuna
dalili zozote za mgomo kutokea.
“Mwanangu alikuwa amelazwa
takribani siku tatu na leo saa 6 ameruhusiwa kurudi nyumbani baada ya
hali yake kuridhisha kwa kweli madaktari wameonyesha ushirikiano mzuri
mpaka kufikia hatua hii,” alisema Suleimani.
Suleiman alisema
licha ya madaktari hao kutoonyesha nia ya kugoma ila wamekuwa
wakiendekeza vitendo vya rushwa jambo ambalo limekuwa likiwasumbua
wakazi mbalimbali wanaofika kupata huduma hiyo hospitalini hapo.
Mwananchi
ambaye hakutaka kutaja jina lake alisema kuwa tangu kutangazwa kwa
mgomo huo Juni 23 mwaka huu yeye hajaona dalili zozote katika hospitali
hiyo ila jambo ambalo linalowasikitisha ni vitendo vya rushwa
vinavyoendelea hapo.
“Sikufichi madaktari wa hapa wanahudumia ila
kama huna fedha utapata shida kwa kiasi fulani na kupelekea mgonjwa
wako kuchukua muda kupata matibabu,” alisema. |
No comments:
Post a Comment