MAHAKAMA
ya Hakimu Mkazi Kisutu, imeamuru upande wa mashtaka kumpa aliyekuwa
Kaimu Mkurugenzi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL),
Theophil Makunga na wenzake wawili maelezo ya malalamikaji ili waweze
kufahamu zaidi kuhusu kesi yao. Makunga anakabiliwa na shtaka
la kuchapisha makala ya kuwashawishi askari na maofisa wa majeshi
nchini kuacha kuitii Serikali. Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu
Mkazi, Waliarwande Lema baada ya Wakili Mwandamizi wa Serikali,
Elizabeth Kaganda kumaliza kuwasomea maelezo ya awali washtakiwa.
Wakili wa utetezi, Gabriel Mnyele aliiomba mahakama hiyo iuamuru upande
wa mashtaka kuwapa washtakiwa hao maelezo ya malalamikaji ili yaweze
kuwasaidia kuifahamu vizuri kesi inayowakabili.
Baada ya
kutolewa kwa ombi hilo, Wakili Mwandamizi wa Serikali, Elizabeth Kaganda
alidai kuwa hana pingamizi na ombi hilo na kwamba atawapatia. Akitoa
uamuzi juu ya ombi hilo, Hakimu Lema aliutaka upande wa mashtaka umpatie
kila mshtakiwa maelezo ya mlalamikaji na kwamba dhamana zao
zinaendelea.
Awali akiwasomea maelezo hayo, Kaganda alidai kuwa
Makunga ambaye ni Mhariri Mtendaji Mkuu wa MCL akikaimu nafasi ya
Mkurugenzi Mtendaji, Novemba 30, 2011 alichapisha waraka wenye kichwa
cha habari 'Waraka Maalumu kwa askari wote', ambao uliandikwa na Samson
Mwigamba kwenye gazeti la Tanzania Daima toleo la 2553. Kaganda alidai
Makunga alifanya kosa hilo kinyume na kifungu cha 32 (1) (c) na 31 (1)
(a) cha Sheria ya Magazeti sura ya 229 iliyofanyiwa marekebisho mwaka
2002.
Akiendelea kuyasoma maelezo hayo ya awali, alidai kuwa
Samson Mwigamba na Abisalom waliwashawishi askari na maofisa wa Jeshi la
Polisi, Magereza pamoja na Jeshi la Ulinzi la Wananchi nchini (JWTZ),
kutoitii Serikali jambo ambalo ni kinyume na kifungu cha 46(b), 55(10(a)
na 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyorekebishwa mwaka 2002.
Inadaiwa
kuwa Novemba 30, 2011, gazeti la Tanzania Daima, toleo namba. 2553
lililochini ya Kibanda (Mhariri Mtendaji), lilichapisha waraka huo ambao
uliandikwa na Samson Mwigamba kupitia safu yake ijulikanayo ‘Kalamu ya
Mwigamba’.
Baada ya Kaganda kusoma maelezo hayo ya awali,
ambayo washtakiwa wote waliyakana na kukubali vyeo na majina yao pekee.
Kaganda aliieleza mahakama kuwa wao watapeleka vielelezo vitatu
ambavyo ni maelezo ya onyo waliyoyatoa washtakiwa polisi, gazeti
lililoandika walaka huo unaodaiwa kuwa ni wa uchochezi na maoni ya
wataalam.
Hakimu Lema aliiahirisha kesi hiyo hadi Agosti 7 ,
mwaka huu itakapoanza kusikilizwa. Makunga alikaimu nafasi ya
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi (MCL) kwa zaidi ya miezi
mitano baada ya aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo Sam Shollei
kumaliza muda wake. Kwa sasa nafasi hiyo inashikiliwa na Tido Mhando.
Awali
Machi 26, mwaka huu, kwa mara ya kwanza alisomewa shtaka hilo
linalomkabili. Makunga anatetewa na Mawakili Mabere Marando na Frank
Mwalongo. Makunga aliachiwa huru baada ya kukamilisha masharti ya
dhamana ya kuwa na wadhamini wawili waliosaini bondi ya Sh5 milioni,
mmoja wa wadhamini hao atoe hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya
kiasi hicho cha fedha na kusalimisha hati yake ya kusafiria mahakamani,
kuripoti polisi mara moja kila mwezi na kutotoka nje ya Dar es Salaam
bila ya kibali cha mahakama.
Februari 15, mwaka huu, Wakili huyo Mwandamizi wa Serikali aliieleza Mahakama kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika. |
No comments:
Post a Comment