Friday, June 22, 2012

Mvuvi ajinasua kinywani mwa kiboko


MVUVI wa samaki katika kijiji cha Butata kata ya Bukima Wilayani Msoma Vijijini mkoani Mara, Stephano Mboyi amenusurika kutafunwa na mnyama aina ya kiboko, baada ya kupambana naye ana kwa ana na kumshinda maarifa.

Tukio hilo ambalo kwa kadri Mboyi mwenyewe alivyolisimulia lilionekana kama ni filamu ya kusisimua ya mpambano baina yake na mnyama huyo hatari lilitokea Jumatatu majira ya saa moja za usiku ziwani.
Akiongea na Mwananchi kwa njia ya simu kutokea katika Hospitali ya Murangi alikolazwa kwa matibabu baada ya kujeruhiwa na mnyama huyo wakati wa pambano hilo, Mboyi alisema alikumbana na tukio hilo wakati akifanya shughuli zake za uvuvi.


“Nilikuwa nimekwenda kutega mtego (nyavu) wangu wa kwa ajili ya samaki aina ya furu. Baada ya kumaliza kuuzungusha, nilianza kuwafukuza samaki kuelekea kwenye mgeto;

“Ghafla nikasikia maji yakifoka kunifuata, nikajua huyo ni kiboko nimeshapatikana. Hivyo ilinibidi nizame ndani ya maji ili nikimbie kando lakini kiboko akataka kunikanyaga, bahati nzuri nikawahi kupita miguuni mwake na nikaenda mbele,” alisema Mboyi.

Aliongeza kuwa wakati anatapatapa akitafuta namna ya kukimbia kutoka ndani ya maji mara kiboko huyo akamsukuma akaanguka na akataka kumkamata mgongoni lakini akakwepa na kuamua kukimbilia kwenye maji marefu.

Aliendelea kusimulia kuwa kiboko huyo alimfuata tena na katika harakati za kupambana naye mara kiiboko akaudaka mkono wake wa kushoto na kuingiza mdomoni mwake.
“Baada ya mkono kuingia mdomoni aliachama zaidi ili anikamate kichwani na kisha anitafune lakini nikamshika kidevu nikamsukuma nikauchomoa haraka mkono wangu kisha nikazama majini,” alieleza Mboyi.

Alisema hatua ya kuzama majini ndiyo iliyokuwa ikimsaidia hivyo aliendelea kuhangaishana na kiboko huyo hata baada ya kuweza kuudaka mkono wake katika kinywa chake kama mara tatu hivi lakini alifanikiwa kujinasua kabla hajatafunwa.

Mboyi alisema kuwa wakati akiendelea kupambana na kiboko huyo watu wakafika ziwani hapo wakiwa na tochi baada ya kusikia kelele.

Alisema yule kiboko alipoona ule mwanga wa tochi, alimwacha yeye kisha akawatisha kuwafukuza wale watu waliokuwa na tochi nao wakakimbia na kisha akamrudia tena na kuanza kusumbuana.Hata hivyo wale watu walirudi tena na kutumia mwanga mkali kummulika kiboko huyo ambapo mara hiyo sasa yule kiboko alimuacha, akasogea nyuma kidogo kisha likawatisha tena kuwafukuza.


Alieleza kuwa hapo ndipo alipopata nafasi ya kukimbia hadi ufukweni upande mwingine, ambapo alikimbia na kiboko huyo kuanza kumfukuzatena, ambapo baada ya mwendo mfupi alianguka ndipo alipobaini kuwa alikuwa amesharudi kwenye maji.

Aliongeza kuwa baada ya hapo ndipo wale watu waliokuwa na tochi walipomfuata na kumchukua na kisha kumpeleka hospitali.

Hata hivyo alisema kuwa katika pambano  hilo aliweza kupata majeraha katika mkono wake wa kushoto tu ambao kiboko huyo alikuwa akiudaoa na kuuingiza kinywani mwake, wakati wa harakati za kujinasua kuutoa mdomoni mwake.

No comments:

Post a Comment