MAWAKILI
 wa Serikali jana waliwasilisha vielelezo Mahakama kuu kuthibitisha 
kwamba umri wa msanii wa filamu Elizabert Michael ni zaidi ya miaka 
18.Habari zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na mawakili wawili;
 mmoja wa Lulu na mwingine wa Serikali ambao hawakutaka kutajwa, 
zimeeleza kuwa vielelezo hivyo vimewasilishwa jana mahakamani hapo.  
 
Habari
 zimeeleza kuwa moja ya vielelezo hivyo vya Jamhuri ni Mkanda wa video 
aina ya CD, yenye mahohjiano kati ya mshtakiwa huyo na mtangazaji mmoja 
nchini.  
"Vingine ni maelezo ya mshtakiwa huyo aliyoyatoa polisi 
wakati alipohojiwa kuhusu tuhuma zinazomkabili, maombi ya hati ya 
kusafiria (Passport) na maombi ya leseni ya udereva, alisema mmoja wa 
mawakili hao. 
 
 
 Awali vielelezo hivyo walitakiwa kuviwasilishwa juzi, lakini ilishindikana na badala yake vikawasilishwa jana. 
 
 Baada
 ya vielelezo kesi hiyo itasikilizwa Juni 25 mwaka huu. Lulu anakabiliwa
 na kesi ya mauaji katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akituhumiwa 
kumuua msanii mwenzake, Marehemu Steven Kanumba aliyefariki dunia 
nyumbani kwake Sinza, April 7, 2012.  
 
Hata hivyo umri wake 
umezua utata baada ya mawakili wake wanaomtetea kudai kuwa bado ni mtoto
 kwa kuwa ana umri wa miaka 17 na si 18 kama hati ya mashtaka 
inavyoonyesha.  
 
Hivyo mawakili hao walilazimika kuwasilisha 
maombi mahakamani kuiomba mahakama iruhusu ufanyike uchunguzi wa umri 
sahihi wa mshtakiwa huyo na ikiridhika kuwa ni mtoto basi kesi yake 
iendeshwe kwa misingi ya kesi za watoto wanaokinzana na sheria ili 
kulinda maslahi yake. 
 
 Juni 11, 2012 Mahakama Kuu ilikubali 
yenyewe kufanya uchunguzi huo kwa lengo la kubaini usahihi wa umri wa 
mshtakiwa huyo na ikaziagiza na kuzipangia tarehe pande zote katika kesi
 hiyo kuwasilisha mahakamani hapo vielelezo watakavyovitumia katika hoja
 zao. 
 
 Jopo la mawakili wanaomtetea Lulu likiongozwa na Kennedy 
Fungamtama Juni 13 waliwasilisha mahakamani hati za viapo vya wazazi 
wake na vielelezo vingine kikiwemo cheti cha kuzaliwa na cha ubatizo 
vinavyoonesha kuwa bado ni mtoto. 
 
 Lakini taarifa zilizopatikana 
mahakamani hapo zinaeleza kuwa vielelezo vilivyowasilishwa na Jamhuri 
vinaonesha kuwa mshtakiwa huyo ni mtu mzima kwa kuwa kwa mujibu wa 
vielezo hivyo ana umri zaidi ya miaka 18.  
 
Viapo vya wazazi wa 
mshtakiwa huyo vilivyowasilishwa mahakamani hapo na Makamu wa Rais wa 
Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Peter Kibatala ambaye ni mmoja wa 
mawakili wanaomtetea Lulu vinaeleza kuwa mshtakiwa huyo ana umri wa 
miaka 17.  
 
Viapo hivyo ambavyo Gazeti hili limefanikiwa kuviona 
ni kiapo cha mama yake Lulu Lucresia Augustin Kalugila, mkazi wa  Dar eS
 Salaam na kiapo cha baba mzazi Michael Kimemeta, mkazi wa Moshi.  
 
Viapo 
 vyote vinaeleza kuwa mshtakiwa huyo alizaliwa April 16, 1995  katika 
kituo cha Afya Muhimbili na kupewa cheti cha kuzaliwa namba B.0318479 
cha Julai 23, 2004.  
Pia viapo hivyo vinaeleza kuwa baada ya kuzaliwa
 mshtakiwa,  mama yake alimpa jina la Diana Michael Kimemeta, lakini 
alimpeleka mtoto huyo Moshi mkoani Kilimanjaro kwa ndugu zake, walimpa 
jina la Elizabeth, jina la bibi yake Elizabeth Shikana.  
 
Viapo 
hivyo vinaendelea kueleza kuwa baada ya majadiliano wote, yeye mama, 
baba na ndugu wengine walikubaliana kuwa wamuite Diana Elizabeth Michael
 Kimemeta .  
 
“ Elizabeth Michael Kimemeta alibatizwa katika 
Kanisa la Katoliki  Chang’ombe Septemba 28, 1997 na alichukua majina ya 
ubatizo Diana Elizabeth Michael Kimemeta;” inasomeka sehemu nyingine ya 
kiapo hicho cha mama wa mshtakiwa.  
 
Utata wa umri wa mshtakiwa 
huyo uliibuka Mei 7, 2012 katika  Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, baada
 ya wakili wake Fungamtama kudai kuwa ana miaka 17 na hivyo kuomba kesi 
yake isikilizwe katika mahakama ya watoto.  
 
Hata hivyo Mahakama 
ya Kisutu iliyakataa maombi hayo ikisema kuwa haina mamlaka ya 
kuyashughulikia na kushauri maombi hayo yawasilishwe Mahamaka Kuu.  
 
Ndipo
 Mei 15 wakili Kibatala aliwasilisha maombi hayo mahakama kuu wakiomba 
mahakama hiyo iamuru kwamba Mahakama ya Kisutu ina uwezo wa kisheria 
kushughulikia maombi hayo.  
Katika maombi hayo namba 46 ya mwaka 
2012,  pia mawakili hao waliomba Mahakama Kuu kama itaridhika kuwa 
mahakama ya Kisutu haina uwezo wa kufanya wala kuagiza uchunguzi huo 
ufanyike, basi Mahakama Kuu yenyewe ama iagize au ifanye uchunguzi huo.  
 
Sambamba
 na hayo pia waliomba Mahakama Kuu iamuru mwenendo wa kesi ya msingi 
katika Mahakama ya Kisutu usimamishwe hadi suala la umri litakapopatiwa 
ufumbuzi.  
 
 
Katika uamuzi wake Jaji Dk. Fauz Twaib alisema kuwa 
Mahakama ya Kisutu ina mamlaka ya kushughulikia maombi hayo na kwamba 
ilikosea kukataa kuyashughulikia.  
 
Pia Jaji Dk. Twaib  
alikubaliana na hoja za pingamizi la awali la wajibu Maombi(Jamhuri) 
kupitia kwa Wakili wa Serikali Shadrack Kimaro akisaidiana na Wakili 
Elizabeth Kaganda, walizozitoa wakati wa usikilizwaji wa maombi hayo, 
Mei 28,2012. 
 
 Wakili Kimaro alidai kuwa maombi hayo 
yamewasilishwa mahakamani hapo kinyume cha sheria na kwamba hata vifungu
 vilivyotumika katika madai hayo haviipi Mahakama Kuu uwezo wa 
kuyashughulikia. 
 Hata hivyo licha ya kukubali kuwa maombi hayo 
yaliwasilishwa mahamakani isivyo sahihi, lakini Jaji Dk. Twaib alisema 
bado Mahakama hiyo ina mamlaka ya kuyashughulikia. 
 
 Chini ya 
kifungu cha 44 cha Sheria ya Mahakama za Hakimu Mkazi, Jaji Dk. Twaib 
aliuagiza upande wa mwombaji(mawakili wanaomtetea mshtakiwa), 
kuwasilisha mahakamani hati hizo za viapo na vielelezo vya umri wa 
mshtakiwa huyo juzi.  | 
    
  
    
  | 
     
No comments:
Post a Comment