Monday, June 11, 2012

Taifa Stars ni leo ama basi


Ni kazi ngumu kwa Taifa Stars kuibuka kiongozi wa Kundi C la michuano ya awali ya Kombe la Dunia kanda ya Afrika kuliko ngamia kupita katika tundu la sindano.
Lakini matumaini yoyote madogo yaliyopo yatafutika kabisa kama timu ya taifa ya soka haitashinda mechi yake nyepesi zaidi ya nyumbani ya kampeni hiyo.

Stars iliyofungwa mabao 2-0 na Ivory Coast katika mchezo wa kwanza wiki-endi iliyopita ugenini, ipo kundi moja pia na Morocco na Gambia inayocheza nayo leo kwenye Uwanja wa Taifa.
Na miongoni mwa timu tatu hizo, nchi hiyo ya Afrika Magharibi ndiyo pekee inayoonekana kuzidiwa uwezo na Stars na isingeweza kucheza nayo wakati muafaka zaidi ya sasa.
Ili kufufua matuamini ya kuongoza Kundi C na kupata nafasi ya kuingia hatua ijayo ya mtoano ya michuano hiyo ya awali, timu ya taifa ni lazima ishinde leo ili isijikute angalau pointi nne nyuma ya timu iliyo kileleni, baada ya raundi mbili na baada ya mchezo kati ya vigogo vilivyopo kundini.
Na ikiwa katika mazingira hayo inakutana na Gambia ambayo ina rekodi nzuri kuliko Tanzania katika ngazi ya michuano ya vijana ya FIFA ikiwa imecheza fainali tatu za dunia kati ya 2005-2009, lakini si kikosi cha kwanza.
Wasiwasi pekee unabaki kwenye malamiko ya kocha Kim Poulsen aliyesema juzi kuwa amesikitishwa na kitendo cha shirikisho la soka (TFF) kutompatia DVD za mechi za Gambia ili ziweze kumsaidia katika maandalizi ya mchezo wa leo.
Pengine TFF ilikwaza na uchache wa mechi za kimataifa ambazo Gambia imecheza.
“Pamoja na kuzikosa DVD hizo nimekiandaa kikosi changu kukabiliana na Gambia na naamini watatumia vizuri uwanja wa nyumbani kwa kushinda mabao mengi,”alisema Poulsen kurejesha matumaini kuwa Taifa Stars itafanya kweli katika mchezo wake pekee ambao itaingia uwanjani ikipewa nafasi kubwa ya kushinda.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment