Monday, July 16, 2012

Gongo iliyoua watu saba ilichakachuliwa


  Ilichanganywa na dawa ya madoa Jik
Wakati Serikali imeeleza kusikitishwa kwake kufuatia vifo vya watu saba vilivyotokana na kunywa pombe aina ya gongo, baadhi ya watu walionusurika wanadai kuwa gongo hiyo ilichanganywa na dawa ya kutakatisha nguo aina ya 'Jik' pamoja na spiriti ili kuongeza ukali.

Baadhi ya watu wakizungumza na NIPASHE Jumapili katika eneo Kigogo Mbuyuni jijini Dar es Salaam jana, walidai pombe hiyo iliyokuwa ikiuzwa na Hekima Lwambano ambaye naye amefariki baada ya kunywa kinywaji hicho, ilikuwa kali sana na harufu mbaya kiasi cha wengine kushindwa kunywa.

Ilielezwa imekuwa ni tabia ya wauzaji wengi wa pombe ya aina hiyo kufanya uchakachuaji wa kuongeza spiriti na Jik kwa wakati mmoja kwa ajili ya kuongeza ukali kitu ambacho kinaweza kuwa hatari endapo viwango vya madawa hayo ikiwa kubwa.


Tukio hilo limekuja siku chache baada ya gazeti hili kutoa taarifa ya uchunguzi ulioelezea kuwepo na utengenezaji wa pombe hiyo wakitumia malighafi hatari ikiwa pamoja na madawa, vyakula vilivyoharibika pamoja na nguo zilizotupwa kwenye madampo mbalimbali. 

Watu waliofariki katika tukio hilo ni Hekima Lwambano, Mzee Kalacha, Harid Hamisi, Methew Mkude maarufu kama `Banzi', Mohamed said, Antipas Kayanmba na Mohamed.

WALIONUSURIKA WANENA

Wakiongea na gazeti hili baadhi ya watu walioathirika walisema imekuwa na nguvu za Mungu kunusurika kwa kifo kwani mara baada ya kunywa pombe hiyo alihisi maumivu makali ya tumbo, mgongo, kiuno na macho kukosa nguvu ya kuona.
Walisema kuna watu wengi wameathirika na pombe hiyo lakini kutokana na wengi wao kunywa na kuondoka sehemu mbalimbali itakuwa sio rahisi kuwatambua.
Mmoja wa walioathirika ambaye alilazwa Hospitali ya Amana (jina linahifadhiwa) alisema yeye alikuwa na kawaida ya kunywa gongo kila mara na hata siku ya tukio alifanya hivyo bila kujua kitu gani kitakachompata.
Aidha mzee Wiilium Msumi (66) ambaye bado amelazwa hospitalini hapo alisema kwa miaka mingi anakunywa pombe ya aina hiyo lakini hajapata tatizo la kiafya, kinachomshangaza mara alipokunywa pombe hiyo alijikuta akibadilika na kusikia maumivu makali.
"lazima watakuwa wameweka kitu, mimi ni mywaji wa gongo kwa miaka mingi lakini kwa haya yaliyotokea inanitia wasiwasi," alieleza.
SERIKALI YAAGIZA MSAKO
Naibu waziri wa Wizara ya mambo ya ndani, Pereira Silima alisema serikali imeagiza jeshi la polisi kuwakamata watu wote wanaomiliki vibanda vya kuuzia pombe hiyo haramu ili wafikishwe katika vyombo vya sheria.
Akiongea wakati alipokwenda kuwajulia hali wafiwa, alisema wananchi washirikiane katika kuwafichua watu wa aina hiyo kwani wanaweza kusababisha maafa makubwa katika jamii kwa kuuza pombe ambayo serikali imepiga marufuku.
Alisema bado serikali inasubiri majibu kutoka kwa mkemia wa serikali, hata hivyo kuna kila dalili kinywaji hicho kilichakachuliwa kabla ya kufikishwa kwa walaji.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment