Wednesday, September 19, 2012

kufuatia utapeli na mke wa kigogo kuhusishwa Usalama wa Taifa waibana polisi


 


Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa,Othman Rashid
NI KUHUSU TUHUMA ZA MKE WA KIGOGO KUTAPELI, MKURUGENZI AMTAKA IGP KUCHUKUA HATUA, MTUHUMIWA AJITETEA
Waandishi Wetu
SAKATA la mke wa kigogo wa polisi kudaiwa kuwatapeli vijana 120 kwa kuwachangisha zaidi ya Sh100 milioni ili awatafutie kazi Idara ya Usalama wa Taifa na Takukuru limechukua sura mpya, baada ya Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Othman Rashid kuwataka polisi wamkamate na kumchukulia hatua za kisheria mwanamke huyo.Utapeli huo wa aina yake, unadaiwa kufanywa na mama huyo kwa kushirikiana na mwanaye (majina tunayo). Pia yumo kijana anayejulikana zaidi kwa jina moja la Baraka ambaye kwenye mpango huo, anajitambulisha kuwa anafanya kazi Ikulu.

Akizungumza na mwandishi wetu Dar es Salaam juzi, Rashid alisema tayari amewasiliana na Mkuu wa Polisi, IGP Said Mwema kuhusu tuhuma hizo ili kujua hatua zilizochukuliwa dhidi yake.
“Nimewasiliana na IGP Mwema ili aweze kunipa ufafanuzi kuhusu mke wa kigogo huyo, lakini nashukuru amenipa ushirikiano na kuniambia kuwa suala hilo wanalishughulikia kisheria zaidi. Watanipa taarifa pindi watakapokuwa wamekamilisha,” alisema Rashid.


Alisema huo ni mfano tu wa baadhi ya watu wanaotumia jina la Usalama wa Taifa kufanya utapeli na kwamba tabia hiyo tayari imewaingiza baadhi ya watu matatani baada ya kukamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria na wengine bado wanatafutwa.

Alisema sheria ni msumeno, hivyo ikibainika mwanamke huyo alijihusisha kutapeli kwa kutimia jina la Usalama wa Taifa, hatua kali zitachukuliwa dhidi yake ili iwe fundisho kwa wengine ambao wanatumia majina ya waume zao kutapeli watu.

Rashid alisema bado ana imani kwamba polisi itamchukulia hatua za kisheria mwanamke huyo ikiwa itathibitika kwamba amejihusisha na utapeli kwa kuwa jeshi hilo lipo kulinda usalama wa raia na mali zao.

Azungumzia tuhuma
Akizungumzia madai hayo jana kigogo huyo wa polisi ambaye mkewe ndiye anayetuhumiwa (jina tunalihifadhi), alisema tangu mwanzo alielewa kwamba anayezungumziwa ni mkewe, lakini akakanusha kuhusika katika utapeli huo.
Alisema kutokana na taarifa ambazo zimekuwa zikiandikwa katika gazeti hili na kumtaja Baraka, vijana wengi waliotapeliwa kutoka mikoa mbalimbali walifunguka akili zao na kubaini kuwa aliyetajwa katika habari ndiye aliyekuwa akichukua fedha kwao.

“Jambo linalonisikitisha ni kwamba, aliyewaletea taarifa hizo za uongo zinazomhusisha mke wangu na utapeli huu ndiye tapeli aliyekuwa akizunguka mikoa mingi nchini kutapeli watu. Hata mke wangu ni mmoja wa waliotapeliwa. Alikusudia kuwapeleka wanafamilia watatu akiwemo mtoto wake, mke wa kaka yake na wifi yake ambaye tunamlea,” alisema.

Alisema mkewe alitoa fedha taslimu zisizopungua Sh1.5 milioni, mbali na gharama za kununua bidhaa na vifaa mbalimbali ambavyo wanafamilia hao wangetakiwa kwenda navyo mafunzoni.
Alisema walishtuka kuwapo dalili za utapeli baada ya watu waliokuwa wakidai kushughulikia ‘mipango’ hiyo kuanza kutoa ahadi zisizotekelezwa, huku wakati mwingine simu zao zikipatikana kwa nadra.

Alipotakiwa kuwataja kwa majina waliokuwa wakishughulikia mipango, ambao walichukua fedha kutoka kwa mkewe kigogo huyo alisema hakumbuki vizuri majina yao. Hata hivyo, alisema mmoja wao anaitwa Baraka.
Mke wa kigogo huyo alikataa kuzungumzia tuhuma hizo akisema: “Hayo yote yapo kwa wakubwa, mimi siwezi kuongelea kitu kilicho ngazi za juu yangu.”

Alipoambiwa kuwa mwandishi wetu amezungumza na mumewe ambaye ameeleza kuwa mama huyo naye ni miongoni mwa waathirika katika utapeli huo, hivyo atoe ufafanuzi alikataa pia kuzungumzia hilo na kukata simu.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah alipotakiwa kuzungumzia tuhuma hizo alisema: “Kwa sasa niko huku Maputo (Msumbiji), siwezi kuzungumzia suala hilo lakini nikirudi nitafutane nitatoa ufafanuzi.”

Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai wa Polisi (DCI), Robert Manumba hakutaka kuzungumzia tuhuma hizo akielekeza atafutwe msemaji wa polisi ambaye simu yake haikupatikana kutwa nzima jana.

Ilivyokuwa
Wiki iliyopita gazeti hili liliripoti habari kuhusu mke wa kigogo kuwatapeli vijana 120 kwa ahadi ya kuwapa ajira katika Idara ya Usalama wa Taifa na Takukuru.

Kati ya Agosti 5 na 7, mwaka huu vijana hao 120 kwa nyakati tofauti walipata taarifa kwamba kuna nafasi za kazi Idara ya Usalama wa Taifa na Takukuru na kwamba nafasi hizo zinapatikana kupitia kwa vigogo wa vyombo vya ulinzi na usalama nchini.

Kwa kupitia kwa mtoto wa mwanamke huyo na kupewa taarifa na rafiki zao, inadaiwa kwamba watu hao ambao wengi wao ni wenye elimu ya chuo kikuu walielezwa kwamba ili kupata kazi hizo ni lazima watoe fedha kati ya Sh700,000 hadi Sh1 milioni.

Walielezwa kuwa mafunzo ya kazi hizo yatatolewa kwa miezi minne katika vyuo vya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), vilivyopo eneo la Mbweni (Dar es Salaam), Zanzibar na Monduli (Arusha).

Siku ya kwanza ambayo waliambiwa kukutana katika viwanja vinavyozunguka uwanja wa zamani wa Taifa, karibu na Ofisi za Baraza la Michezo Tanzania (BMT), ili wapelekwe Mbweni kwa ajili ya kupangiwa vituo vyao vya kazi walielezwa kwamba baadhi yao majina yao yalikuwa hayajaingizwa katika mfumo. Baada ya wiki moja  walitakiwa kukutana tena eneo hilo ili kupelekwa, lakini walielezwa kuwa wangepelekwa Septemba 2, mwaka huu kwa kuwa baadhi yao hawakuwa na namba.

Ilipofika Septemba 2, vijana hao wakati wakielekea Mbweni, walielezwa kuwa muda umekwenda na hawataweza kupokewa katika kambi hiyo hivyo kupangishiwa nyumba za kulala wageni zilizopo Tegeta.
Hadi walipofika katika Ofisi za Mwananchi, Ijumaa wiki iliyopita, bado baadhi yao walikuwa wanaishi katika nyumba hizo na wengine kupewa nauli ili warudi katika mikoa waliyotoka kwa maelezo kuwa nafasi zitatangazwa gazetini Oktoba 3, mwaka huu.

Habari zilizolifikia gazeti hili zimeeleza kuwa polisi imefungua jalada kuhusu tuhuma hizo na tayari limewahoji watu kadhaa Dar es Salaam na mikoani, lakini mke wa kigogo huyo hajahojiwa.

No comments:

Post a Comment