Monday, November 18, 2013

Moshi polisi academy mabingwa mchezo wa Judo

Na Dixon Busagaga wa Globu ya jamii,Moshi

KLABU ya Mchezo wa Judo chuo cha taaluma ya polisi Moshi (MPA) imefanikiwa kuchukua ubingwa wa jumla katika mashindano ya kwanza ya mchezo huo yaliyofahamika kama First Moshi Polisi Academy Judo Championship 2013.

Katika mashindano hayo yaliyoandaliwa na Chuo cha Polisi kwa kushirikana na chama cha mchezo wa Judo nchini ilishuhudiwa wachezaji chipukizi kutoka vilabu vya Korogwe, Kisutu na Moshi Polisi wakionesha vipaji vyao huku mchezaji wake chipukizi, Andrew Thomae akiibuka mchezaji bora wa mashindano.

Klabu ya Moshi Polisi ilifanikiwa kuibuka mshindi wa baada ya wachezaji wake kutawala mapambano ya uzito wa kilo 60, 66, 73 pamoja na mapambano ya wazi yaani Open huku klabu ya Korogwe ikifanikiwa kushika nafasi ya pili.

Mchezaji Thomae wa MPA ambaye ndiye chachu ya ubingwa wa MPA, alianza kuonesha ubabe wake mbele ya mpinzania wake Dola Abeid ambaye pia anatoka klabu ya MPA akimwangusha mara kadhaa ndani ya dakika 3:34:05 za mchezo.

Thomae pia alifanikiwa kumbwaga mchezaji Abubakar Magogo katika mchezo wa fainali ambaye awali alimduwaza bingwa wa Judo Afrika mashariki Geofrey Mtawa kutoka klabu ya magereza Ukonga katika hatua ya nusu fainali mchezo ambao hata hivyo uliisha kwa Mtawa kurusha lawama kwa muamuzi kuwa hakutendewa haki.

Akizungumza na Globu ya jamii baada ya mchezo kumalizika, Mtawa alisema kuwa kimsingi alichokifanya mwalimu wake ni kinyume na sheria za mchezo kwani alimnyima pointi za wazi ambazo zingepelekea yeye kutangazwa mshidni kwa kile alichodai kuwa Mwamuzi huyo kuwabeba “Madogo”.

“Huu ni uonevu, pale kilichotokea ni uonevu, mimi nimetumia tekniki za mchezo nimemnyanyua dogo ndani ya uwanja nikamwangusha chini tena ameangukia mgongo lakini cha kushangaza mwamuzi ananinyima pointi eti nimenyanyua nje ya uwanja, hapana mchezo huu hautakuwa kwa staili hii, wananishushia hadhi yangu,” alisema Mtawa.

Washindi wengine katika mapambano mengine ni Bakari Magogo kilo 60 (MPA), Mohammed Korogombe kilo 73 (MPA), Gervas Chilipueli, kilo 81 (Korogwe), Amina Mohammed mpambano wa wazi (MPA) na Geofry Mtawa kilo 90.

Zawadi katika mashindano kwa mshindi wa kwanza katika uzito wa 60 hadi 90 ni vyeti, vikombe, medali na fedha taslimu ambapo washindi wote walizawadiwa zawadi zao na mgeni rasmi Kamanda wa Polisi Mkoani Kilimanjaro, ACP-Robert Boaz.

Mashindano hayo yalidhaminiwa na Mkuu wa Chuo cha MPA, Matanga Mbushi kwa kushirikiana na kampuni ya Marenga Investment, Ibra Line, Tanzanite One, pamoja na Benki ya NMB tawi la Mandela .
Washiriki wa mashindano ya mchezo wa Judo wakiwa katika picha ya pamoja.
Moja ya pambano la mchezo wa Judo kwa uzito wa kilogramu 73.
Wanawake pia walioneshana kazi katika mashindano hayo .
Mwanamuziki wa zamani wa bendi ya Twanga Pepeta Anko Venna akitoa burudani katika mashindano hayo ,Venna hivi sasa ni miongoni mwa waongozaji wa Bendi ya Super Kwata International pinayomilikiwa na chuo cha Polisi.
Mgeni rasmi katia mashindano hayo kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro Robert Boaz(mwenye kofia nyekundu)akifuatilia moja ya pambano.
Bingwa wa mchezo wa judo Afrika mashariki Geofrey Mtawa wa magereza Ukonga akijaribu kutaka kumtupa mchezaji Abubakary Magogo wa MPA katika pambano la wazi ambalo hata hivyo Mtawa alipoteza kwa pointi.
Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro Robert Boaz akikabidhi zawadi kwa mshindi wa kwanza wa mchezo wa Judo Geofrey Mtawa wa magereza Ukonga kwa wachezaji wa uziti wa kilogramu 90.
Mchezaji bora wa mchezo wa Judo katika mashindano ya First Moshi Poilisi Academy Judo Championship 2013,Andrew Thamae akiwa ameshikilia vikombe alivyo fanikiwa kutwaa,kulia kwake ni kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro Robert Boaz aliyekuwa mgeni rasmi.

No comments:

Post a Comment