Friday, August 1, 2014

Ebola inaenea kwa kasi ya kutisha



Zaidi ya watu 700 wamefariki kutokana na Homa ya Ebola kanda ya Afrika Magharibi
Shirika la afya duniani linasema kuwa ugonjwa wa Ebola unaendelea kuenea kwa kasi ya kutisha.
Mkuu wa shirika hilo, Margaret Chan ameambia mkutano wa viongozi wa kikanda kuwa ikiwa watakosa kuudhibiti utasababisha janga la kuogofya kwa binadamu.
Hata hivyo amesema kuwa ugonjwa huo ambao umesababisha maafa utaweza kudhibitiwa ikiwa mpango mzuri wa kufanya hivyo utakuwepo.
Shirika hilo limezindua mpango wa thamani ya dola milioni 100 kupambana na mlipuko wa homa ya Ebola katika kanda ya Afrika Magharibi.
Mkurugenzi mkuu Margaret Chan anakutana na Marais wa Guinea, Liberia na Sierra Leone nchini Guinea kudurusu hali ya maambukizi katika nchi hizo.
Ramani ya nchi zilizoathirika kutokana na Ebola
Zaidi ya watu mia saba wamefariki kutokana na Ebola katika nchi hizo tangu mwezi Februari.
Shirika hilo linasema kuwa wataalamu zaidi wa matibabu wanahitajika katika kanda hiyo ikiwa juhudi za kupambana na ugonjwa huo zitafanikiwa.
Shirika hilo limepongeza juhudi zilizochukuliwa hadi sasa kukabiliana na ugonjwa huo ingawa haijulikani namna ambavyo baadhi ya jitihada kama vile kuwatenga wagonjwa zitaweza kutekelezwa
Awali, Rais wa Liberia, Ellen Johnson-Sirleaf aliambia BBC kuwa mlipuko wa ugonjwa huo ni janga kubwa.
Serikali yake imejipatia siku 60 kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo.

No comments:

Post a Comment