Thursday, June 7, 2012

Ang'atwa na mbwa katika gereji ya Wachina

Beatrice Mmari (32), amejikuta katika wakati mgumu baada ya mbwa anayemilikiwa na kampuni ya Wachina, ya Spring City Enterprises, inayojihusisha na shughuli za gereji, eneo la Kijitonyama, jijini Dar es Salaam, kumvamia na kumng’ata kwenye mguu wake wa kushoto.

Tukio hilo lilitokea jana saa 4 asubuhi katika gereji hiyo iliyopo eneo hilo, wakati mama huyo alipofuata gari lake alilolipeleka hapo kwa ajili ya matengenezo.



Akizungumza na NIPASHE, Beatrice alisema alifika eneo hilo muda huo na kwamba, wakati akiangalia gari lake lililokuwa mita chache kutoka walipo mbwa hao, ghafla alishitukia aking’atwa na mbwa nyuma ya mguu wake wa kushoto.


Alisema mbwa huyo alimtoboa sehemu ya mguu huo baada ya kuchana nguo yake kwa meno.


Mama huyo alisema aliokolewa na mmoja wa Wachina aliyekuwa karibu, ambapo alikimbilia kwenye gari lake.


Alilaani kitendo cha Wachina hao cha kutokujali utu wa mtu kwa kutoonyesha kusikitishwa, baada ya kumwambia mama huyo aende mwenyewe hospitali kutibiwa.


“Jambo linalonisikitisha zaidi…baada ya kung’atwa hawakuonyesha kunijali, huku  wakiniambia niende mwenyewe hospitali,” alisema Beatrice.


Mama huyo alikwenda katika Hospitali ya AAR iliyopo Mtaa wa Chato Regent Estate, Mikocheni.


Meneja wa Biashara wa Kampuni hiyo, Yu, alipoulizwa na NIPASHE iwapo wana utaratibu wa kuchanja mbwa wake chanjo ya kichaa cha mbwa, alisema hawajawahi kuwafanyia hivyo.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment