Thursday, June 14, 2012

Fifa yawabeba Mwape, Asamoah


UONGOZI wa klabu ya Yanga umehofia panga la Shirikisho la Soka la Kimataifa ‘FIFA’ katika harakati zake za kutaka kuwatema wachezaji wake wawili wa kimataifa Davis Mwape pamoja na Kenneth Asamoah ambao msimu uliopita walishindwa kuonyesha cheche zao.

Woga huo wa viongozi ahao wa Yanga umekuja mara baada kukumbuka msukosuko walioupata kutoka FIFA baada ya kumtema beki John Njoroge wakati akiwa bado ana mkataba wa kuitumika klabu hiyo na kushindwa kumlipa haki zake.

Hivi karibuni mara baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu baadhi ya viongozi wa Yanga walisikika wakisema kuwa watawatema Mwape na Asamoah kwenye usajili wa msimu ujao kutokana na wachezaji hao kuonyesha kiwango cha chini.

Akizungumza na Mwananchi jana Katibu Mkuu wa Yanga, Celestine Mwesigwa alisema kuwa ndoto za kuvunja mkataba na wachezaji hao hazipo na watandelea kuitumika hadi pale watakapokuwa wamemaliza mikataba yao.

“Mwape na Asamoah bado ni wachezaji wetu na hatuna mpango wa kuwatema kwa sababu bado tuna imani nao na wataendelea kuitumika klabu yetu hadi watakapokuwa wamemaliza mikataba yao,” alisema Mwesigwa.

Hata hivyo habari za uhakika kutoka ndani ya klabu hiyo zinasema kuwa uongozi wa Yanga umeshindwa kufikia uamuzi huo wa kukatisha mikataba ya wachezaji hao kutokana na kutokuwa na fedha za kuwalipa kama ilivyokuwa kwa Njoroge ambaye hadi sasa hajalipwa madai yake licha ya FIFA kuitaka Yanga kumlipa mchezaji huyo raia wa Kenya.

Mwape na Asamoah wote kwa pamoja bado wana mkataba wa mwaka mmoja wa kuitumikia Yanga ambayo msimu uliopita ilishika nafasi ya tatu na kukosa nafasi ya kushiriki katika mashindano ya kimataifa.

Wakati huo huo klabu ya Yanga imeweka bayana majina  ya wagombea ambao wamepitishwa kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika klabu hiyo, mpaka jana mchana hakuna pingamizi lolote ambalo limewasilishwa.

Kamati ya uchaguzi ya Yanga, juzi ilibandika majina  ya waliopitishwa kuwania kinyang’anyiro hicho ambacho uchaguzi wake umepangwa kufanyika Julai 15 jijini Dar es Salaam.

Hata hivyo kuna habari kuwa uchaguzi huo utafanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, huku taarifa za chini kwa chini zikidai kuwa wagombea Ally Mayai ‘Tembele’ na Sara Ramadhani ni miongoni mwa watakaowekewa pingamizi.

Mmoja wa wanachama wa Yanga alisema kuwa Tembele watamuwekea pingamizi kwa madai kuwa alijiuzuru kwenye uongozi uliopita kabla ya kumaliza muda wake huku Sara wakimtuhumu kwa masuala mbali mbali.

Katibu wa kamati ya uchaguzi, Francis Kaswahili alisema kuwa mpaka jana mchana hawajapokea pingamizi lolote na ameonya wanachama kutowasilisha mapingamizi feki kwa sababu ya chuki binafsi na atakayebainika kufanya hivyo atatozwa faini ya Sh500,000 sambamba na kufungiwa kwa miaka miwili kujihusisha na masuala ya soka.


No comments:

Post a Comment