Thursday, June 21, 2012

James Mbatia alia na misamaha ya kodi

Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia
Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia, ameitaka serikali kuangalia upya misamaha ya kodi inayotolewa kwa taasisi zisizo za kiserikali ili iweze kumsaidia mwananchi masikini.


Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama hicho, alikuwa akichangia mjadala wa bajeti ya mwaka 2012/2013 iliowasilishwa Alhamis iliyopita na Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa.

Alihoji kuhusiana na misamaha ya kodi ambayo imekuwa ikitolewa na serikali kwa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali kama inalenga katika kumsaidia malalahoi.

Alitoa mfano wa Taasisi ya Aghakhan, ambayo imekuwa ikipata misamaha ya kodi tangu serikali ya awamu ya kwanza.

“ Je, hosptali za Aghakhan zimekuwa zikitoa huduma bora zaidi, aghali zaidi je, zinamsaidia mlalahoi,” alihoji.

Alisema kama serikali itaamua kuwapa misamaha wazawa wa hapa nchini ni wazi kuwa itaongeza uzalishaji nchini na kutoa fursa ya ajira kwa watu wengi.

“Kama mkiwasaidia wazawa kama 200 wakawa kama Reginald Mengi (Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP), wakaweza kuzalisha ajira za watu 500 mtakuwa mmepunguza tatizo la ajira kwa kiasi kikubwa,” alisema.

Pia alisema bajeti hiyo imeshindwa kuonyesha ni jinsi gani itaondoa msongamano wa magari katika jiji la Dar es Salaam.

Mbatia alisema katika twakimu zinaonyesha kuwa foleni hiyo imekuwa ikisababisha upotevu wa Sh. bilioni nne kila siku.

Alisema fedha hizo zinapotea kutokana na mafuta yanayopotea njiani, uchafuzi wa mazingira na muda wa kazi.

Alisema ni vyema kusikiza michango ya wabunge na kwenda kuangalia upya kwa kuifanyia marekebisho bajeti waliyoiwasilisha.


No comments:

Post a Comment