Monday, June 11, 2012

Msaidieni mtoto Said

Baada ya Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kumruhusu mtoto Saidi Adam (11) kurejea nyumbani kutokana na tatizo linalomkabili kuonekana kuwa kubwa kwao, hivi sasa mtoto huyo anahitajika kupatiwa matibabu nje ya nchi ili kuokoa maisha yake.
Akizungumza na Nipashe Jumamosi jana, baba wa mtoto huyo, Adam Said alisema kwa sasa wapo nyumbani kwa mwenyeji wao Makonde Mbezi Beach jijini Dar es Salaam, wakiwa hawajui la kufanya kutokana na Muhimbili kushindwa kutatua tatizo.

“Tumeambiwa mirija ya kupumua na ile ya maji kuelekea kwenye moyo imeziba, hivyo kusababisha tatizo la kukua kwa moyo ambao sasa unaonekana umekuwa na mapacha,” alisema Adam.
Hata hivyo, Adam alisema baada ya kulazwa kwa takribani siku 10 katika hospitali hiyo, madaktari walitoa dawa ili ziweze kupunguza uvimbe wa tumbo, lakini si kwa kutibu tatizo linalomkabili Said.
Alisema kutokana na tatizo hilo, anawaomba wasamaria wema wajitokeze kumsaidia mtoto wake kuweza kusafirishwa nje ya nchi kwa ajili ya kutibiwa tatizo hilo na aweze kurejea katika hali ya kawaida.
“Kwanza kabisa nawashukuru watu mbalimbali waliojitokeza kumsaidia Said kupitia kwa wahusika wa gazeti hili, na wale ambao walinichangia ili kuweza kulazwa hospitalini kuangaliwa tatizo lake..Mungu atawalipa zaidi na ninawaomba wengine wajitokeze kufanya hivyo,” alisema.
Alisema watu ambao wanahitaji kumsaidia Saidi ili kumwezesha kufanikisha matibabu yake hususani nchini India, wanaweza kutumia akaunti namba 0152303111100 CRDB tawi la Mikocheni kwa jina la Hadija Abdallah Mkwinda, ama ofisi za gazeti hili.
Saidi ni mtoto kutoka kijiji cha Mbaya wilayani Liwale mkoani Lindi ambaye anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo tangu Agosti 2008 na kumsababishia tumbo lake kukua siku hadi siku.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment