Monday, June 11, 2012

RC apiga marufuku malori kubeba abiria

MKUU wa Mkoa wa Tanga, Chiku Gallawa, amepiga marufuku magari ya mizigo kubeba watu kwenda kwenye mikusanyiko ya watu wengi, ikiwamo misibani na harusini lengo likiwa ni kuepusha maafa yanayotokana na ajali.

Agizo hilo limekuja baada ya kukithiri kwa vifo vitokanavyo na ajali za barabarani, ambazo husababishwa na magari ya mizigo kubeba watu kwenda misibani, maharusini na minadani.
Mwaka jana watu 24 walipoteza maisha na wengine 39 kujeruhuiwa na kupata ulemavu wa maisha.
Akizungumza kwenye kikao cha wadau wa usafirishaji na wamiliki wa magari ya mizigo juzi, Gallawa alisema kuanzia sasa ni marufuku magari ya mizigo kubeba watu na kuwapeleka  katika mikusanyiko.

Gallawa alisema imekuwa kawaida kwa watu wa Tanga kutumia magari ya mizigo kwenda katika shughuli za jamii na kusahau maafa ambayo yanaweza kutokea, huku wakiacha usafiri wa mabasi.

 “Kuanzia sasa ni marufuku kwa magari ya mizigo kubeba watu na kuwapeleka katika sherehe au misibani, tunashuhudia maafa ya mara kwa mara yanayotokana na ubebaji watu kwenye malori, sasa basi!” alisisitiza Gallawa.

Aliwata wakazi wa mijini na vijijini kuacha kutumia usafiri huo, kwani umekuwa ukipoteza roho za watu wengi na watumie mabasi ambayo ndiyo wenye haki za kisheria kubeba abiria.
Kuhusu tabia ya baadhi ya madereva kuweka miti na majani barabarani gari linapoharibika, Gallawa alisema watu hao wamekuwa wakichafua mazingira kwani gari hilo likitengenezwa hawaondoshi uchafu huo.

Alisema tabia hiyo imekuwa kero na wakati mwingine husababisha ajali bila sababu za msingi, hivyo kila kijiji kinatakiwa kuwa na walinzi ambao watanakili namba za magari yanayofanya hivyo.
 


No comments:

Post a Comment