Tuesday, July 17, 2012

Kigogo UVCCM auawa mkutanoni

  18 watiwa mbaroni, kufikishwa kortini
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kata ya Ndago Wilaya Iramba mkoani Singida, Yohana Mpinga (30), ameuawa baada ya kutokea vurugu katika mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Kamanda wa Polisi Mkoa Singida, Kamshina Msaidizi wa Polisi, Linus Sinzumwa, alisema tukio hilo lilitokea saa 10:00 jioni katika kijiji cha Ndago.

Alisema siku hiyo, Chadema walikuwa na mkutano wao halali, lakini wakati wakiendelea, kulizuka vurugu kubwa kati ya wafuasi wa chama hicho na wa CCM.

Kwa mujibu wa Kamanda Sinzumwa, mawe na fimbo zilitumika kwenye vurugu hizo.
Alisema mkutano huo ulikuwa ukihutubiwa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, Mwita Waitara na Kitila Mkumbo.

Alisema baada ya vurugu kupamba moto, marehemu alikimbia hadi kwenye nyumba ya mwalimu Shume Lyanga, lakini alifuatwa ndani na watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa Chadema na kuadhibiwa hadi kifo.
Watu 18 wametiwa mbaroni kutokana na tukio hilo na polisi wamesema watachujwa kubaini wahusika halisi ili wapandishwe kizimbani kujibu tuhuma za mauaji.


Hata hivyo, habari zaidi kutoka eneo la tukio ambazo zimekanushwa na Kamanda Sinzumwa, zinasema kigogo na kiongozi mmoja wa CCM aliwakodi vijana kutoka jirani na eneo la mkutano kwa lengo la kuleta vurugu ili mikutano ya Chadema isifanyike.
Inasemekana kuwa kigogo huyo aliwakodishia gari dogo aina ya Hiace na kuwagharimia malazi, chakula na kuwalewesha kwa pombe.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) Mkoa wa Singida, Joseph Isango, alisema chama chake hakihusiki na vurugu hizo, kwani eneo la tukio wafuasi wake walivumilia sana, kabla ya kutokea vurugu.
Wakati huo huo, Chadema imekanusha kuhusika na vurugu hizo.
Ofisa wa Sera na Utafiti wa Chadema, Waitara Mwikwabe, alisema chama hicho kiliandaa mikutano ya hadhara katika Jimbo la Iramba Magharibi na kwamba mikutano hiyo ilitolewa taarifa polisi na mkuu wa polisi kutoa baraka zote kama utaratibu wa sheria unavyotaka kwa barua yenye kumb. Na KIO/BI/1/VOL.V/268 ya Julai 12, mwaka huu.
Waitara alisema vurugu zilitokea wakati wakijiandaa kuanza hotuba, ndipo vijana wapatao wanane walianza chokochoko kwa kutoa lugha ya matusi na punde mawe yakaanza kurushwa kutoka sehemu mbalimbali.
Alisema hadi wanamaliza mkutano huo uliokuwa wa amani na utulivu baada ya kuondolewa vijana hao, wazungumzaji walijenga hoja juu ya mustakabali wa jimbo na taifa kwa ujumla.
Aliongeza kuwa wananchi waliohudhuria walitaka viongozi wa Chadema waendelee kuhutubia, lakini walibanwa na ratiba ya kuwahi mkutano wa pili, Kinampanda.
Hata hivyo, Waitara alisema walitoa taarifa kituo kidogo cha polisi Ndago kwa kufungua jalada na kupewa RB namba NDG/RB/190/2012 ambapo waliwataja baadhi vijana waliowatuhumu kuhusika katika vurugu hizo.
Vijana waliofunguliwa mashitaka katika kituo hicho ni pamoja na Daniel Sima, Tito Nitwa, Bakili Ayubu, Yohana Makala Mpande, Ernest Kadege, Simion Makacha, Anthony John na Frank Yesaya.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment