Sunday, October 9, 2016

RAIS AHUTUBIA TAMASHA LA MADHEHEBU YA BOHORA

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

Simu : +255-22-2114512, 2116898
Email : press@ikulu.go.tz
Tovuti : www.ikulu.go.tz
Faksi : 255-22-2113425
OFISI YA RAIS,
IKULU,
1 BARABARA YA BARACK OBAMA,
11400 DAR ES SALAAM,
TANZANIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 08 Oktoba, 2016 amehutubia katika tamasha la madhehebu ya Bohora ambayo yanafanya maadhimisho ya dunia ya sikukuu ya mwaka mpya wa Kiislam Jijini Dar es Salaam.
Maadhimisho hayo yamewaleta nchini wafuasi zaidi ya 30,000 kutoka nchi mbalimbali duniani na kuongozwa na Kiongozi Mkuu wa Madhehebu ya Bohora Duniani Mtukufu Dkt. Syedna Mufaddal Saifuddin Saheb (TUS).
Akihutubia wafuasi wa Bohora katika Msikiti wa Hakimi uliopo Upanga Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli amemshukuru Kiongozi Mkuu wa Bohora kwa kukubali kufanya maadhimisho ya mwaka mpya wa madhehebu hayo hapa nchini na amewashukuru na kuwapongeza wafuasi wa madhehebu hayo kwa kukubali kuja hapa nchini na kukaa kwa siku zote za maadhimisho yaani kuanzia tarehe 02 Oktoba, 2016 walipoanza hadi tarehe 11 Oktoba, 2016 watakapomaliza.
Rais Magufuli, amewapongeza viongozi na wafuasi wa madhehebu ya Bohora kwa kutumia maadhimisho haya kuhimiza amani, upendo na mshikamano na pia amewashukuru kwa kushiriki katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi ikiwemo mchango Dola za Marekani 53,000 zilizotolewa na Kiongozi Mkuu wa Bohora kwa Serikali kwa ajili ya kuchangia kampeni ya utengenezaji wa madawati, na kuwaleta madaktari kutoka Hospitali ya Saifee ya India waliotoa matibabu bure kwa wananchi wa Arusha.
Aidha, Rais Magufuli amewakaribisha wafuasi wa Bohora duniani kuja kuwekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali zikiwemo Kilimo, Uvuvi, Misitu, Mifugo, Madini na Gesi kwani soko la uhakika lipo ndani ya nchi, katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) yenye watu takribani milioni 400.
Kwa upande wake Kiongozi Mkuu wa Madhehebu ya Bohora Dkt. Syedna Mufaddal Saifuddin Saheb (TUS) amemshukuru Rais Magufuli kwa kuungana na wafuasi wa madhehebu ya Bohora katika maadhimisho hayo na amesema wafuasi wote wa Bohora wanahimizwa kushirikiana na mamlaka zilizopo katika nchi wanazoishi, kuwa raia wema na kufuata sheria.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam

No comments:

Post a Comment