Monday, June 25, 2012

Azma ya walimu kugoma yashika kasi

Sakata la walimu kutangaza azma ya kugoma limeendelea kushika kasi ambapo walimu katika wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza wamesema wako tayari kukatwa mishahara yao iwapo serikali itaona hiyo ndiyo njia sahihi ya kuwazuia wasigome.

Akitangaza azma hiyo wakati wa kikao cha makubaliano ya kuungana na wenzao nchi nzima kushiriki mgomo huo, Katibu wa Chama cha walimu wilayani humo, Josephat Mashinji, alisema ofisi yake ilipokea waraka wa mgomo kwa nchi nzima tangu Mei 13, mwaka huu. 

Alisema kuwa waraka huo umetoa notisi ya siku 30 hadi Julai 8, mwaka huu kuitaka serikali itekeleze matakwa yao mbalimbali vinginevyo wataitisha mgomo usio na kikomo kwa nchi nzima.

Alisema kwa kuzingatia waraka huo wako tayari kukatwa mishahara yao katika kipindi chote cha mgomo iwapo serikali itaona ndiyo njia sahihi ya kuzuia mgomo huo. Alisema hatua hiyo inatokana na ukweli kuwa hivi sasa wanatambua haki zao za kikatiba na wako tayari kuzipigania.

Kwa mujibu wa Mashinji, hivi sasa CWT kipo katika mgogoro na serikali utakaodumu hadi Julai 8, mwaka huu, na endapo serikali haitaridhia, chama hicho kitatangaza mgomo wa walimu kutokwenda kazini.

Miongoni mwa madai yao, walimu wanataka nyongeza ya mshahara kwa asilimia100, asilimia 55 ya posho kwa walimu wa masomo ya Sayansi, asilimia 30 kwa walimu wanaofundisha katika mazingira magumu na asilimia 50 kwa walimu wa masomo ya sanaa.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment