Monday, July 9, 2012

Mgomo wa madereva 18 washikiliwa na polisi

Jeshi la polisi mkoani Kilimanjaro, linawashikilia watu 18 wenye umri kati ya miaka 18-20 kwa tuhuma za kuhusika kwenye vurugu za mgomo wa madereva wa daladala waliokuwa wanapinga ongezeko la ushuru.
Kaimu Kamanda wa mkoa wa Kilimanjaro, Koka Moita, alisema watu hao wanasadikiwa kuwa ni vibaka waliojitokeza wakati wa mgogoro huo kwa lengo la kujipatia maslahi yao binafsi.

Alisema, kutokana na vurugu hizo, magari mawili yaliharibika na watu watatu waliokuwa kwenye gari namba T 703 AGQ walijeruhiwa na kupelekwa hospitali ya Mkoa ya Mawenzi.

Imedaiwa kuwa vijana hao walikuwa wakifanya fujo zikiwemo kuwashusha abiria kwenye magari ambayo yalitii amri ya manispaa ya ongezeko la ushuru na kuwachapa viboko.

Hata hivyo, Moita alisema, kabla ya ongezeko hilo daladala zilikuwa zinalipa Sh. 1000, na mabasi Sh 1500 kama ushuru wa maegesho lakini kwa sasa katika sheria iliyopitishwa na manispaa iliwataka kulipa Sh 1500 kwa daladala, na Sh 2000 kwa magari makubwa, jambo ambalo lilileta mgogoro mkubwa.

Kaimu kamanda alisema kuwa, jeshi la polisi haliusiki na kitu chochote katika mgogoro unaoendelea kati ya manispaa na wadau wa usafi, lakini wataendelea kuweka doria ili kuhakikisha hakuna vurugu yoyote inayoendelea mpaka muafaka utakapopatikana.
CHANZO: NIPASHE JUMAPI

No comments:

Post a Comment