Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju 
Na Jacquiline Mrisho-MAELEZO, Dodoma
MWANASHERIA
 Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju amewataka Mawakili wa Serikali kuwa
 makini na kutoa ushauri kwa uadilifu na uweledi wa hali ya juu pindi 
wanapotoa ushauri wa kisheria kuhusu mikataba mbalimbali.
Mhe.
 Masaju ameitoa kauli hiyo alipokuwa akiongea  na Mawakili  wa Serikali 
wakati wa ufunguzi wa mafunzo yanayohusu uhakiki wa mikataba ya ununuzi 
wa umma leo Mjini Dodoma.
Alisema
 ni vyema wakatekeleza jukumu hilo kwa makini kwani ushauri unaotolewa 
na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupitia mawakili hao ndio 
msimamo wa Serikali.
“Ninapenda kuwakumbusha kwamba ninyi
 ni watumishi wa umma na mnaongozwa na Sheria ya Utumishi wa Umma ya 
mwaka 2002 pamoja na kanuni zake za mwaka 2003” alisema Mhe. Masaju na 
kuongeza kuwa:
“Kama walivyo watumishi wengine wa umma na kwa msingi huu, ninyi ni sehemu ya Serikali na nafasi yenu katika Serikali ni kubwa”.
Pia aliwataka wanasheria wa Serikali kujengewa
 uwezo kuhusu uhakiki wa mikataba na iwapo watashindwa kutekeleza wajibu
 huo ipasavyo watawajibishwa kwa kuchukuliwa hatua stahiki za kinidhamu.
Alisema
 kuwa kutokana na kuongezeka kwa thamani ya mikataba inayohakikiwa na 
wanasheria wa taasisi  ya manunuzi ni wazi kwamba kuna umuhimu wa 
Maafisa Sheria kupatiwa mafunzo hayo.
“Wanasheria
 wa Serikali wanaohakiki mikataba hii wanawajibika kuzingatia sheria 
zinazohusiana na mikataba husika pamoja na maadili ya Wanasheria wa 
Serikali katika Utumishi wa Umma kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 
27 cha Sheria ya Utekelezaji wa Majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa
 Serikali ya mwaka 2005”,alisema Mhe. Masaju.
Mhe.
 Masaju alishauri utaratibu wa mikataba yote kuhakikiwa Dar es Salaam 
ubadilike kwani unasababisha ongezeko la gharama kwa taasisi za Serikali
 na kuchelewesha miradi.
Alifafanua kuwa Divisheni
 ya Mikataba iko Makao Makuu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali 
pekee hivyo, mikataba yote ya mikoani ni lazima ipelekwe Dar es Salaam 
kwa ajili ya kuhakikiwa.
“Hii
 inasababisha wadau hasa wa kwenye Halmashauri za Wilaya, Miji, 
Manispaa, Jiji na wengine walioko mikoani kusafiri na kupeleka mikataba 
Dar es Salaam kwa ajili ya uhakiki” alisema Mhe. Masaju.
Hivyo
 alisema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeona umuhimu wa 
kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali wa Ofisi za Mwanasheria Mkuu wa 
Serikali zilizoko Mikoani ili hatimaye baadhi ya Mikataba kutoka kwa 
wadau walioko wilayani na mikoani iwe inapelekwa katika Ofisi za 
Mwanasheria Mkuu wa Serikali zilizoko mikoani.

No comments:
Post a Comment