Friday, June 15, 2012

Dereva wa lori jela kwa kuchakachua mafuta


Na Daniel Mjema,Moshi
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi mkoani Kilimanjaro,imemhukumu kifungo cha miaka miwili jela, dereva wa lori moja la mafuta baada ya kupatikana na hatia ya kuchakachua mafuta aina ya disel.

Awali upande wa mashitaka ukiongozwa na wakili wa serikali kanda ya Moshi, Jullius Semali ulidai kuwa mshitakiwa huyo, Winter Aloyce Mushi alitenda kosa hilo Agosti 17 mwaka 2011.

Ilidaiwa siku hiyo,akiwa na lori hilo likiwa na lita 37,000 mali ya kampuni ya Panone & Company Ltd, mshitakiwa alichakachua lita 6,000 za mafuta aina ya Diesel yenye thamani ya sh12,630,000.

Akisoma hukumu hiyo jana mjini Moshi, Hakimu Mkazi Munga Sabuni alisema mahakama hiyo imeridhika bila shaka yeyote na ushahidi uliotolewa na mashahidi watano wa upande wa mashitaka.

Sabuni alifafanua kuwa ushahidi wa mashahidi hao akiwamo mmoja kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa huduma ya Nishati na Maji (Ewura), ulithibitisha mafuta hayo yalikuwa yamechakachuliwa.

“uchunguzi wa kimaabara ulionyesha kiwango cha density (ubora) kilikuwa kimeshuka kutoka 831 hadi 827 na hakuna mtu mwingine aliyekuwa amekabidhiwa mafuta hayo zaidi ya mshitakiwa”alisema.

Hakimu huyo alisema kuwa kwa kuwa vitendo vya uchakachuaji mafuta vimekuwa na athari kimazingira na vyombo vya moto,mahakama inamhukumu kifungo cha miaka miwili jela ili iwe fundisho kwa wengine.
 

No comments:

Post a Comment