Tuesday, June 26, 2012

Kuondoa kodi za bodaboda kwazua mjadala



 UAMUZI wa Serikali kuondoa kodi ya mapato kwa wafanyabiashara wa kusafirisha abiria kupitia pikipiki maarufu kama bodaboda, umepokelewa kwa hisia tofauti na  wananchi hasa baada ya kutolewa hoja wengi, wanaonufaika na biashara hiyo sio vijana wanaoendesha bali ni wamiliki ambao wengi wao ni maofisa , wafanyabiashara wakubwa na watumishi wa sekta nyingine.

Naibu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), Hezron Kaaya alisema Serikali inapaswa kutumia vyombo vyake ili kufanya uchunguzi ni kina nani wamiliki wa bodaboda badala ya kufikia uamuzi ya jumla kuondoa kodi.


Alisema kama Serikali ina nia ya dhati kuwasaidia, waendesha bodaboda ilazimishe wawe na mikataba na waajiri na wawalipe vizuri tofauti na sasa ambapo wanatakiwa kuwafikishia wamiliki wa  bodaboda kati ya Sh 15,000 na 20,000 kwa siku na wao wakijitafutia kipato nje ya fedha hizo.
 “Sisi hatupingi kufutwa kodi ila tunataka Serikali itazame biashara hii kwa ujumla wake ili kweli iwasaidie vijana”alisema Kaaya.
 Alisema Serikali inachopaswa kufanya ni kuongeza wigo wa kupata watu wengi wanaolipa kodi kwani sasa wafanyakazi wa umma ndio wanapata shida kwa kulipa kodi ya mishahara ya Payee kubwa na wao ndio sasa walipa kodi wakubwa.

Naye Ismail Kayanda alifafanua kuwa, hoja ya kuondolewa kodi hiyo, inakuwa na manufaa kwani vijana wengi wamejiajiri katika kazi ya bodaboda na kuwa na vipato vya uhakika.

Kayanda alisema tangu biashara ya bodaboda ianze makundi ya vijana, wasio na ajira ambao walikuwa kero hasa nyakati za usiku, imepungua.

“Hapa Dodoma ulifika wakati ukitembea usiku unakuwa na hofu ya kukumbwa na vijana  lakini sasa vijana hao hao, tunawaona wametulia wanafanyakazi ya bodaboda,”alisema Kayanda.

Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, akihitimisha hotuba ya bajeti, alieleza kukubaliana na hoja ya wabunge, ikiwamo kamati ya Uchumi na Fedha ambayo ilishauri kuondolewa kwa kodi hiyo na pia kodi kwa wafanyabiashara wadogo au vipato vyao havijafikia 3 milioni.

No comments:

Post a Comment