Sunday, June 10, 2012

Wizara ya Habari yaijia juu TEF


SIKU moja baada ya Jukwaa la Wahariri (TEF) kutokuwa na imani na Wizara ya  Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, imekuja juu na kukanusha madai ya Jukwa la hilo kwamba msuguano baina ya viongozi wakuu wa wizara unakwamisha kupatikana kwa sheria ya vyombo vya habari nchini.

Kauli ya wizara imekuja siku moja baada ya TEF kusema hawana imani na Waziri wa Wizara hiyo, Dk Fenella Mkangala na Katibu Mkuu wake Sethi Kamuhanda, kama wanaweza kufanikisha kupatikana kwa sheria hiyo kutokana na msuguano baina yao.



Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam, Kamuhanda alisema hana ugomvi wala msuguano wowote na waziri wake na kuongeza kuwa wanaelewana na wanafanya kazi vizuri na kudai kuwa ameshangazwa na taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari.

Alisema haiwezekani watu wenye uadilifu wakagombana wakati ni watu makini katika kazi zao na wanaelewana hata kwenye kazi zao.

“Mkumbuke kuwa sisi hatuna mgogoro wowote kwa sababu waziri kipindi alipokuwa naibu waziri tulifanya kazi kwa pamoja hivyo nashangaa mimi na waziri wangu kuona vyombo vya habari vinaripoti kuwa tuna mgogoro kati ya mimi na waziri,” alisema na kuongeza:

“Mimi sio mtu wa migogoro  kwa watu wanaonifahamu kwa sababu sina sababu ya kugombana na waziri wangu hili nataka kila mmoja wetu ajue,” aliongeza.
Katibu huyo Mkuu alikiri kupokea mwaliko wa kufungua na kufunga Mkutano wa Mwaka wa Wahariri wa Vyombo  vya Habari pamoja na Baraza la Habari na kusema kuwa alipata udhuru na kutoa taarifa kwa Katibu Mkuu wa Baraza la Habari nchini (MCT) Kajubi Mukajanga.
“Nilitakiwa nije kwa niaba ya waziri lakini tukaletewa taarifa za vikao vya kamati ya bunge vinaanza na mimi ndiye muandaaji mkuu wa vikao hivi, hivyo nilishindwa kuja na nilitoa taarifa kwa katibu wa MCT  lakini nashangaa kuona taarifa hizi zimekuja tofauti ….muulizeni huyo katibu kama sikuongea naye,” alisema.

Aliongeza: “Mimi nilizungumza nao juu ya hali ya dharura iliyojitokeza kwa hiyo sikuwa na sababu ya kuwakimbia," alisema.

Kufuatia hatua hiyo katibu huyo mkuu alisema wizara haitachukua hatua yoyote kuhusiana na taarifa iliyotolewa na Jukwaa la Wahariri pamoja na baraza la Habari nchini (MCT).
Katika hatua nyingine, Serikali imepongeza jukwaa la Wahariri nchini kwa  kuwezesha kazi ya uandishi wa habari kufanyika kwa kuzingatia maadili, wajibu na waledi wa kitaaluma.
Pia Katibu huyo  Kamuhanda alisema Jukwaa hilo kwa kuimarisha weledi wa kitaaluma, uwajibikaji, utendaji wa kazi, uhuru wa vyombo vya habari pamoja na kujenga mfumo wa usimamizi wa maadili ndani ya vyombo vya habari.

Tamko la TEF linatokana na viongozi hao kualikwa kwenye mkutano huo ambao pamoja na mambo mengine ulijadili Mchakato wa Sheria ya Haki ya Kupata Habari na Huduma za Vyombo vya Habari nchini, ambao umekuwa ukisuasua kwa takriban miaka 10 sasa.

Taarifa ya TEF na kusainiwa na Katibu wake Neville Meena, ilisema azimio hilo lilitolewa na wahariri watendaji wa vyombo vya umma, vinavyomilikiwa na mashirika ya dini pamoja na watu binafsi katika mkutano uliofanyika Morogoro kati ya Juni 3 mpaka 5.
Inasema kuwa, vitu vingine muhimu vilivyokuwa vinajadiliwa ambavyo vilihitaji viongozi kutoka wizarani kuwepo ni pamoja na, kuwezesha kazi ya uandishi wa habari kufanyika kwa kuzingatia maadili, wajibu na weledi wa kitaaluma.

Pia  kuimarisha weledi wa kitaaluma, uwajibikaji utendaji wa kazi, na uhuru wa vyombo vya habari na zaidi kujenga mfumo wa usimamizi wa maadili ndani ya vyombo vya habari.
Taarifa hiyo ilisema kuwa, wanachoomba ni dhana  ya kutekeleza jambo hilo ambayo ni Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari na Sheria ya Haki ya Kupata Habari, ambazo mchakato wake umedumu kwa zaidi ya miaka 10 sasa bila kupatikana.

No comments:

Post a Comment