Tuesday, July 15, 2014

Kafulila akebehi waliomshtaki, NCCR Kigoma waandamana


Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), akiwahutubia wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Community Center uliopo Mwanga Manispaa ya Kigoma/Ujiji. PICHA:JONCTAN NGELLY.
Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila, amesema hajapata taarifa rasmi za kufunguliwa kesi ya madai ya Sh. bilioni 310 mahakamani, lakini akasema hashangazwi na hatua hiyo kwa kuwa hata wasio haki wanao ujasiri wa kushtaki.

Pia mamia ya wafuasi wa Chama cha NCCR Mageuzi wamefanya maandamano ya amani katika Manispaa ya Kigoma/Ujiji kudai vigogo wa serikali wanaodaiwa kushirikiana na mmoja wa watu, ambao Kafulila anawatuhumu kuiba fedha katika akaunti ya Escrow ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuzirudisha, wakamatwe na kufikishwa mahakamani.

Kafulila amefunguliwa kesi hiyo namba 131/2014 na Kampuni ya kuzalisha umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na wenzake wawili, anaodaiwa kuwatuhumu kuiba Sh. bilioni 200 kwenye akaunti ya Escrow ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Walalamikaji wengine katika kesi hiyo iliyofunguliwa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, ni Kampuni ya Pan Afrikan Power Solutions Limited (PAP) na Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni hiyo, Harbinder Sigh Seth.

Kafulila alisema hayo katika taarifa aliyoituma kwa NIPASHE kupitia mtandao wa kompyuta jana, ikiwa ni siku moja baada ya baadhi ya magazeti nchini kuripoti habari za walalamikaji hao kumfungulia kesi hiyo mahakamani wiki iliyopita.

“Nimesikia magazetini kwamba nimefunguliwa kesi na Kampuni ya PAP inayodai kumiliki IPTL kwamba nimewachafua ndani na nje ya Bunge. Kwanza Watanzania waelewe kuwa hata wasio haki wanao ujasiri wa kushtaki, ndiyo maana hata Yesu alishtakiwa na hata Nyerere alishtakiwa,” alisema Kafulila.

NCCR-MAGEUZI WAANDAMANA KIGOMA
Wakati Kafulila akisema hivyo, mamia ya wafuasi wa Chama cha NCCR Mageuzi wamefanya maandamano ya amani katika Manispaa ya Kigoma/Ujiji kudai vigogo wa serikali wanaodaiwa kushirikiana na mmoja wa watu, ambao Kafulila aliwatuhumu kuiba fedha katika akaunti hiyo kuzirudisha, wakamatwe na kufikishwa mahakamani.

Maandamano hayo yalifanyika juzi, majira ya saa nane mchana, kuanzia uwanja wa Ndege, uliopo eneo la Katubuka hadi kwenye uwanja wa Community Center Mwanga katika manispaa hiyo na kufanya mkutano wa hadhara.

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa, wakiongozwa na Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi, Mosena Nyambambe, Mbunge wa Muhambwe (NCCR-Mageuzi), Felix Mkosamali, Katibu Mkuu mstaafu wa chama hicho, Samuel Ruhuza, na Kafulila.

Waandamanaji walibeba mabango yaliyoandikwa ujumbe mbalimbali, huku wakiimba wimbo wa “Tunataka fedha zetu,” “Tukaneni matusi, yakiisha yote, rudisheni fedha zetu,”  “Tumechoka kudhulumiwa na serikari ya CCM.”

Pia walikuwa wakiimba “Tumeanza leo hapa manispaa, tutakwenda Kigoma Kusini, Kigoma Kaskazini, Kasulu, Kibondo tunakwenda kuamsha watu waelewe wajibu wao kwa taifa lao”.

Akizungumza na wananchi jana kwenye mkutano wa hadhara, Kafulila alisema hana imani na Takukuru kama itasaidia, kwani siyo mara ya kwanza wanafanya uchunguzi kuhusu ufisadi wa IPTL na Ikulu inakalia ripoti.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment